IQNA

Sheikh wa Msikiti Mkuu wa Paris asema mwaka 2025 ulikuwa mgumu zaidi kwa Waislamu Ufaransa

14:51 - January 04, 2026
Habari ID: 3481766
IQNA – Sheikh Chems-Eddine Hafiz, mlezi wa Msikiti Mkuu wa Paris, amesema mwaka 2025 ulikuwa miongoni mwa miaka migumu zaidi kwa Waislamu nchini Ufaransa, ukitawaliwa na matukio ya vurugu yaliyofikia kiwango cha “kuuawa kwa misingi ya dini.”

Katika ujumbe wake, alieleza kuwa mwaka uliopita ulikuwa wa aina ya pekee, “miaka inayojichora ndani ya miili na akili,” kutokana na ukubwa wa changamoto zilizokabili jamii ya Kiislamu nchini humo. Alitaja mauaji kadhaa ya Waislamu, huku akilaani ukimya wa mamlaka za Kifaransa mbele ya matendo hayo.

Sheikh Hafiz alikumbusha mauaji ya kikatili ya kijana Mwislamu aliyeuawa akiwa anaswali msikitini, uhalifu uliochochewa na chuki za kidini na ubaguzi wa rangi. Alieleza kuwa aliyekuwa Waziri wa Ndani wa mrengo wa kulia, Bruno Retailleau, alipuuzia tukio hilo kwa kutofika msikitini wala kuifariji familia ya marehemu, hali iliyozua hasira kubwa ndani ya jamii ya Kiislamu. Familia ya marehemu ilikataa kumpokea Retailleau alipojaribu kufanya ziara siku mbili baadaye.

“Aliuawa kwa sababu alikuwa Mwislamu. Kifo chake kilikutana na ukimya wa haraka, kana kwamba maisha ya baadhi ya watu yanaweza kufutwa kwa urahisi kuliko ya wengine. Ukimya huo uliacha alama nzito zaidi ya huzuni ya wapendwa wake,” alisema Hafiz.

Aliongeza kuwa mwaka huo pia ulijaa matukio mengine ya mauaji kwa misingi ya kidini na ubaguzi wa rangi, ikiwemo kisa cha mhamiaji wa Kitunisia aliyeuawa kwa risasi na polisi wa Kifaransa. Aidha, alionyesha wasiwasi kuhusu kuongezeka kwa chuki dhidi ya Uislamu (Islamophobia) nchini Ufaransa, akisema imefikia viwango ambavyo havijawahi kushuhudiwa.

Sheikh Hafiz alieleza kuwa hali hiyo inaleta “hali ya uchovu wa kila siku” kwa Waislamu, unaojumuisha mashaka, mitazamo ya dharau na umbali wa kijamii, hali ambayo imekuwa ya kawaida na imewacha uchovu wa kimaadili kwa wengi.

Katika wito wake, alihimiza wananchi wa Ufaransa “kuacha kukana uhalisia huu, kuupuuza au kuupunguza katika mijadala ya umma.” Alisisitiza kuwa lengo si kutafuta huruma maalum, bali kukabiliana na ukweli kwa uwazi na uaminifu, bila kupotosha au kuupamba. Ujumbe huu ulielekezwa kwa wanasiasa wa mrengo wa kulia na wa mrengo mkali wa kulia, pamoja na vyombo vya habari vinavyoshirikiana nao, ambavyo vinachochea chuki na ubaguzi.

Kwa mujibu wa Hafiz, jamii ya Kiislamu nchini Ufaransa imeonyesha “ushikamanifu mkubwa na Jamhuri na misingi yake.” Hata hivyo, baadhi ya wanasiasa na watengenezaji maoni huwatendea kana kwamba si sehemu ya muundo wa kijamii wa Kifaransa, hali ambayo alisema ni “ya kutia wasiwasi kwa sababu inapingana na simulizi rahisi na inalazimisha kufikiria kwa undani zaidi.”

Kwa upande mwingine, wanasiasa wa wastani nchini Ufaransa wanahusisha kuongezeka kwa uhasama dhidi ya wahamiaji na Uislamu na hotuba za wanasiasa fulani waliokita mizizi katika ajenda za uhamiaji, akiwemo Bruno Retailleau wa chama cha mrengo wa kulia Les Républicains, pamoja na Marine Le Pen na msaidizi wake Jordan Bardella wa chama cha mrengo mkali wa kulia National Rally, ambao wamegeuza uhasama dhidi ya wahamiaji,  hususan wenye asili ya Kiislamu, kuwa nguzo kuu ya siasa zao nyembamba za uchaguzi.

3495953

Kishikizo: waislamu ufaransa
captcha