IQNA

Jeshi la Yemen lashambulia kituo cha Aramco nchini Saudia

13:41 - April 15, 2021
Habari ID: 3473817
TEHRAN (IQNA)- Jeshi la Yemen limetangaza kuwa vikosi vyake vya angani na makombora vimetekeleza oparesheni ya pamoja kwa kutumia makombora saba na ndege zisizo na rubani au drone na kulenga kituo cha kusafisha mafuta cha Aramco mkoani Jizan nchini Saudia.

Katika taarifa Alhamisi Asubuhi, Msemaji wa Majeshi ya Yemen Brigedia Jenerali Yahya Saree amesema: "Aramco na maeneo mengine yamelengwa kwa kutumia makombora saba aina ya Sa'ir na Badr. Kwa uwezo wake Mwenyezi Mungu maeneo hayo yamelengwa kwa ustadi na kusababisha moto katika kituo hicho cha mafuta."

Saree ameongeza kuwa, ndege zisizo na rubani aina ya Samad-3 na Oasef-2k pia zimetumiwa katika oparesheni hiyo.

Amesema maeneo hayo yamelengwa baada ya muunganoo vamizi unaoongozwa na Saudia kushadidisha mashambulizi, msingiro na jinai dhidi ya watu wa Yemen hasa jinai ya hivi karibuni dhidi ya raia eneo la Sa'ada.

Halikadhalika amesema Jeshi la Yemen litaendeleza oparesheni zaidi ndani ya Saudia iwapo ufalme huo hautasitisha vita na mzingiro dhidi ya watu wa Yemen.

Siku ya Jumatano jeshi vamizi la Saudia lilidondosha mabomu katika wilaya ya Monabeh katika mkoa wa Sa'ada kaskazini mashariki mwa Yemen ambapo kwa uchache watoto wawili waliuawa na wengine wanne kujeruhiwa.

Yemen inasema kuwa ni haki yake kujihami kutokana na uvamizi wa Saudi Arabia na magenge yake na maadamu uvamizi huo ungalipo, miji ya Saudia nayo haitobaki salama.

Mwezi Machi 2015, Saudi Arabia ikiungwa mkono na Marekani, UAE na nchi zingine kadhaa iliivamia kijeshi Yemen na kuiwekea mzingiro nchi hiyo wa nchi kavu, baharini na angani ambao unaendelea hadi sasa.

Vita hivyo vya Saudia vimesababisha maafa makubwa zaidi ya kibinadamu nchini Yemen.

Kwa mujibu  Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu (OCHA),  vita vya Saudi Arabia dhidi ya Yemen vimepelekea zaidi ya watu 233,000 kupoteza maisha katika kipindi cha miaka sita iliyopita. Idadi kubwa ya raia hasa wanawake na watoto ni waathirika wakuu wa hujuma za Saudia dhidi ya Yemen.

Hivi karibuni, Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) lilisema kati ya Januari na Juni 2021, asilimia 54 ya Wayemen, yaani watu milioni 16.2, watakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula kutokana na vita vya Saudia dhidi ya nchi hiyo.

/3964730

captcha