Hujjatul Islam Javad Sadiqzadeh, mshauri wa Meya wa Jiji la Tehran na mkuu wa Kituo cha Mausla ya Kidini cha Baraza la Jiji la Tehran amesema vituo vya kuchanja COVID-19 vitakuwa vinafanyakazi jioni katika misikiti yote kwa lengo la kutoa chanjo baada ya Sala ya Ishaa.
Mpango huu utaendelea hadi Novemba 16 kwa lengo la kuwafikia wale ambao hawajafika katika vituo vya chanjo.
Mbali na kutoa chanjo misikitini Baraza la Jiji la Tehran pia lina mabasi maalumu yanayozunguka kwa ajili ya kutoa chanjo na halikadhalika pia katika treni ya chini ya ardhi au Metro kuna vituo 22 vya kutoa chanjo ya COVID-19.
Kwa mujibu wa Wizara ya Afya ya Iran watu zaidi ya milioni 48 nchini wamepata chanjo ya kwanza ya COVID-19 kati ya watu wote milioni 83 nchini huku wengine milioni 24 wakiwa wamepata dozi kamili ya chanjo hiyo.
Chanjo za COVID-19 zinazotumika kwa wingi nchini Iran hivi sasa ni pamoja na Sinopharm, AstraZeneca, na COVIran Barekat.