IQNA

Jinai dhidi ya Waislamu

Waumini 87 wauawa katika hujuma ya kigaidi msikitini Peshawar, Pakistan

18:13 - January 30, 2023
Habari ID: 3476489
TEHRAN (IQNA)- Watu wasiopungua 87 wameuawa katika shambulizi la kujilipua kwa bomu lililotokea katika msikiti wa mji wa Peshawar huko kaskazini magharibi mwa Pakistan.

Vyombo vya usalama vya Pakistan vimeripoti kuwa, Waislamu wasopungua 87 wameuawa shahidi na zaidi ya 160 wengine wamejeruhiwa katika mlipuko kubwa uliotokea ndani ya msikiti wa mji wa Peshawar. 

Maafisa wa hospitali za mji huo wanasema idadi ya waliofariki dunia huwenda ikaongezeka kutokana na idadi kubwa ya majeruhi wa hujuma hiyo. 

Afisa wa polisi ya mji wa Peshawar, Sikandar Khan, amewaambia waandishishi habari kwamba mlipuko huo umetokea wakati idadi kubwa ya Waislamu walipokuwa wamekusanyika kwa ajili ya ibada ya Swala. Khan ameongeza kuwa: "Sehemu moja ya jengo la msikiti huo imeanguka, na watu kadhaa wanaaminika kuwa chini ya vifusi vyake".

Maafisa wa usalama wanasema, gaidi aliyetekeleza hujuma hiyo alikuwa kwenye safu ya mbele wakati alipojilipua na kuwajeruhi makumi ya waumini waliokuwa wakitekeleza Sala ya Adhuhuri.

Mkuu wa polisi ya Peshawar, Muhammad Ijaz Khan, amesema katika taarifa yake kwenye televisheni ya Pakistan kwamba msikiti huo ulikuwa na uwezo wa kuwa na karibu watu 300 na ulikuwa umejaa wakati wa mlipuko huo.

Duru zinadokeza kuwa kundi la Taliban la Pakistan linalojulikana Kiurdu kama Tehreek-e-Taliban Pakistan ( TTP) limedai kuhusika na shambulizi hilo katika ujumbe wa Twitter.

Waziri Mkuu wa Pakistan, Shehbaz Sharif amelaani shambulizi hilo na kuamuru vyombo husika kuhakikisha matibabu bora zaidi yanatolewa kwa waathiriwa. Vilevile ameahidi kuchukua "hatua kali" dhidi ya wale waliohusika na shambulio hilo.

3482275

captcha