Rose Hamid, 56, siku ya Ijumaa alikuwa katika mkutano wa kampeni wa Trump kwa lengo la kulalamikia hatua ya mwanasiasa huyo tajiri kutoa matamshi yaliyo dhidi ya wakimbizi Waislamu kutoka Syria.
Trump alipomuona Bi. Hamid aliwataka polisi wamtimue kutoka katika mkutano huo.
Baada ya kutimuliwa katika mkutano huo wa kampeni, Bi. Hamid alisema alifika katika mkutano huo ili kuwaonyesha washiriki taswira halisi ya mwanamke Mwislamu. Ameongeza kuwa alisimama wakati wa mkutano huo ili ampe Trump na wafuasi wake fursa ya kumuona mwanamke aliyevalia Hijabu. Ameongeza kuwa wafuasi wa Trump walimzingira na kumvunjia heshima kama mwanamke mwislamu.
Kufuatia hujuma za kigaidi za Paris, Ufaransa na San Bernardino Marekani, Trump alitaka Waislamu wasiruhusiwe kukanyaga ardhi ya Marekani. Msimamo huo mkali wa Trump amepelekea kuibuka wimbi jipya la chuki dhidi ya Uislamu Marekani. Aidha mwanasiasa huyo anayewania kuwa rais wa Marekani alitaka kutumiwe mbinu za manazi wa Ujerumani chini ya uongozi wa Adolph Hitler dhidi ya Waislamu.