IQNA

Mbaguzi Trump aalikwa msikitini afunzwe Uislamu

16:40 - January 18, 2016
Habari ID: 3470057
Kiongozi wa Chama cha Leba cha nchini Uingereza, Jeremy Corbyn amemualika mbaguzi Donald Trump anayewania kuteuliwa na chama cha Republican kugombea urais nchini Marekani atembelee msikiti mjini London, huenda akapata somo.

Gazeti la Guardian limemnukulu Corbyn akisema: "Nimeamua kumwalika Donald Trump atakapotembelea Uingereza, afuatane na mimi hadi katika jimbo langu kwa sababu naona ana matatizo na Wamexico na Waislamu.”

Corbyn amesema hayo baada ya kuzuka mjadala katika bunge la Uingereza wa kujadili iwapo Trump aruhusiwe kuingia nchini humo au la.

Mkuu huyo wa chama cha Leba cha Uingereza amesema, kwa mtazamo wake haoni haja ya kuzuiwa Donald Trump kuingia nchini humo, na iwapo atambelea Uingereza anapenda ampeleke msikiti akapate somo.

Amesema: Kama unavyojua, mke wangu mimi ni Mmexico na jimbo langu ni jimbo lenye watu wa makabila na tamaduni nyingi tofauti, sasa nitakachofanya ni kumchukua Trump hadi msikitini katika jimbo langu, ili aweze kuzungumza na watu humo.

Kufuatia hujuma za kigaidi za Paris, Ufaransa na San Bernardino Marekani, Trump alitaka Waislamu wasiruhusiwe kukanyaga ardhi ya Marekani. Msimamo huo mkali wa Trump amepelekea kuibuka wimbi jipya la chuki dhidi ya Uislamu Marekani.

3458812

captcha