Ayatullah Sayyid Ali Khamenei aliyasema hayo leo mjini Tehran katika muendelezo wa vikao vya
sikukuu ya Nairuzi alipoonana na majimui ya viongozi wa serikali, wajumbe
wa kamati kuu ya Majlisi ya Ushauri ya Kiislamu (Bunge la Iran) viongozi
wa ngazi za juu wa chombo cha Mahakama na viongozi wa taasisi na asasi
nyingine nchini na huku akiwashukuru viongozi hao hususan viongozi wa
serikali kwa juhudi na kazi kubwa inayofanywa na serikali katika
utekelezaji wa siasa za uchumi usioyumba wa kimuqawama, amelitaja suala
la kudumisha mapenzi na maelewano pamoja na umoja na mshikamano baina ya
viongozi nchini kuwa ni jambo muhimu sana katika ufanikishaji wa siasa
hizo.
Ameongeza kuwa kituo kikuu cha kuendeshea uchumi usioyumba wa
muqawama inabidi kisimamiwe na serikali bali na Makamu wa Kwanza wa Rais
mwenyewe na sambamba na kuvutia ushirikiano na msaada wa vyombo na
taasisi nyingine zote, kituo hicho kikuu kinapaswa kifuatilie kwa kina
harakati na kazi za sekta tofauti na kutoa uungaji mkubwa kwa sekta ya
uzalishaji wa bidhaa za ndani pamoja na kuandaa mazingira ya kuchukuliwa
hatua kubwa na za pande zote kwa ajili ya kufanikisha uchukuaji hatua
na utekelezaji wa kivitendo wa siasa za uchumi wa kimuqawama.
Amesema,
nafasi ya kusimamia kituo kikuu cha uchumi wa kimuqawama ni muhimu mno
katika suala zima la kuchunguza na kufuatilia kwa kina kazi za taasisi
na vyombo mbali mbali na kuongeza kuwa: Katika ufuatiliaji huo wa kina,
inabidi taasisi zote zinazofanya kazi katika kalibu na fremu ya siasa za
uchumi wa kimuqawama zitiwe nguvu, na zile taasisi ambazo zinapuuza na
hazishughulishwi na siasa hizo, inabidi ziingizwe kwenye mkondo wa
kufanikisha siasa hizo na wakati huo huo vizuiwe vitendo vya taasisi na
vyombo ambavyo vinakwenda kinyume na uchumi wa kimuqawama.
Kiongozi
Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza kuwa, hatua na vitendo
katika uchumi wa kimuqawama inabidi viwe kwa namna ambayo itakapofika
mwishoni mwa mwaka huu (wa Kiirani wa 1395 Hijria Shamsia), kuweze
kutolewa ripoti ya kina na ya kivitendo kuhusiana na kazi zilizofanyika
katika nyuga tofauti za ufanikishaji wa uchumi huo.
Ameongeza kuwa:
Majimui ya taasisi za utekelezaji na utendaji nchini Iran, zinao uwezo
wa kufanikisha siasa za uchumi wa kimuqawa na Majlisi ya Ushauri ya
Kiislamu (Bunge) nayo ina wajibu wa kuisaidia serikali katika suala
hilo.
Ayatullah Udhma Khamenei ameongeza kuwa: Tunachotaka sisi si
kupandisha juu matarajio na matumaini yetu kwa serikali na tunatambua
matatizo na changamoto mbali mbali zilizopo, lakini kunaweza kufanyika
mambo makubwa kupitia kubana matumizi katika baadhi ya sekta kwa ajili
ya kujaza mapungufu na nakisi zilizoko katika sekta nyinginezo.
Amesema,
majimui ya viongozi nchini ni ya watu muhimu sana katika jamii ambao
wana uzoefu na wana msukumo mkubwa wa kazi na fikra nzuri na ni
wachapaji kazi. Ameongeza kuwa: Kituo kikuu cha kuendeshea siasa za
uchumi ya kimuqawama ni kituo cha kifikra na pia cha amali na vitendo na
kinapaswa kutumia vizuri uwezo wa viongozi nchini na pia kistafidi
vilivyo na uwezo na suhula zilizopo katika asasi na vyombo mbali mbali
nchini kwa ajili ya kuchukua maamuzi sahihi na kutekeleza kivitendo
maamuzi hayo.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza
pia kuwa, kazi ya kuendesha nchi, jukumu ambalo ni la serikali na
hususan mheshimiwa rais mwenyewe ni kazi nzito sana na kuongeza kuwa:
Kutokana na mheshimiwa rais kuzongwa na kazi na majukumu mengi, badala
yake Makamu wa Kwanza wa Rais ambayo ana nafasi ya juu serikali anaweza
kutoa mchango maalumu na wa kipekee katika kuongoza kituo kikuu cha
uchumi wa kimuqawama.
Ayatullah Udhma Khamenei amesisitiza kwamba:
Mimi nitaunga mkono vilivyo hatua yoyote ile ya Serikali, ya Bunge na ya
Chombo cha Mahakama ambayo itakuwa kwa hakika inalenga kuwahudumia
wananchi na kutatua matatizo yao; lakini kwa sharti kwamba ihisike kuwa
kazi inayofanyika ni ya lazima na ina manufaa kweli kwa taifa.
Amesisitiza
kuwa: Utekelezaji wa siasa za uchumi wa kimuqawama, inabidi utegemee
kikamilifu uwezo na suhula zote zilizopo nchini na ambazo si kidogo.
Vile
vile Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa Marekani
ni nembo ya tabia mbaya na ahadi zisizo na mwamana na kuongeza kuwa:
Wamarekani hawaaminiki hata kidogo, na ukiwaweka pembeni Wamarekani,
kuna baadhi ya nchi za Magharibi ambazo nazo ni vivyo hivyo haziaminiki,
hivyo tunapaswa kutegemea uwezo wetu wenyewe. Aidha amesema: Misimamo
na hatua zinazochukuliwa na viongozi wa Marekani nazo zinathibitisha
uhakika huo.
Ayatullah Udhma Khamenei amesema kwa kusisitiza kuwa,
iwapo tutaingia kiikhlasi na kiukweli katika medani ya ufanikishaji wa
siasa za uchumi huo, basi bila ya shaka yoyote Mwenyezi Mungu
atatusaidia na atakuwa pamoja nasi. Ameongeza kuwa: Katika njia ya
maisha ya mtu binafsi na ya jamii nzima kiujuma, siku zote kuna
misukosuko na panda shuka nyingi, lakini lililo muhimu ni kuwa, watu
wote na katika mazingira yoyote wawayo, wanapaswa kuhakikisha kuwa
hawaisahau na wala hawatoki nje ya njia ya asili.
Amesema, ni jambo
la lazima kulipa umuhimu na uzito wa hali ya juu suala la kuisaidia na
kuiunga mkono sekta ya uzalishaji wa ndani na kuongeza kuwa: Lazima
uzalishaji uzingatiwe vilivyo na upewe kipaumbele maalumu katika sekta
zake zote mbili, sekta ya viwanda na sekta ya kilimo.
Kiongozi
Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amelitaja suala la mafahamiano,
mapenzi na mshikamno baina ya viongozi kuwa ni mambo yanayoandaa uwanja
wa kufanikiwa uchumi wa kimuqawama na kusisitiza kuwa: Hakuna jambo
lolote litakaloweza kufanyika bila ya kuweko ushirikiano baina ya
viongozi wote.
Ayatullah Udhma Khamenei ameongeza kuwa: Jamhuri ya
Kiislamu ya Iran siku zote imekuwa na bahati nzuri ya kuwa na umoja wa
kitaifa, lakini pambizoni mwa umoja huo wa kitaifa, inabidi yaweko pia
mapenzi na mshikamano baina ya viongozi na kwamba umoja na mshikamano
huo haukinzani hata kidogo na suala la kuweko watu wenye mitazamo na
fikra tofauti katika jamii.
Aidha amesema, mkutano huo wa leo ni
dhihirisho la wazi la mapenzi na mafahamiano, ukuruba na kushibana
viongozi nchini na kuhimiza kuwa: Inabidi viongozi nchini na licha ya
kuwa na fikra na mitazamo tofauti washikamane vilivyo katika
ufanikishaji wa malengo makuu ya Mapinduzi ya Kiislamu.
Kiongozi
Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza pia kuwa: Leo hii humu
nchini kuna hisia kuwa viongozi wa mihimili mitatu mikuu ya dola
(Serikali, Bunge na Mahakama) pamoja na viongozi wakuu wa mfumo wa
Jamhuri ya Kiislamu wana fikra na mtazamo mmoja kuhusu wajibu wa
kufanikisha malengo makuu ya Mapinduzi ya Kiislamu licha ya kuwa na
fikra tofauti na kutofautiana juu ya njia za kufanikisha malengo hayo.
Katika
sehemu nyingine ya hotuba yake, Ayatullah Udhma Khamenei ametoa
shukrani zake nyingi kwa watu wa familia za viongozi nchini hususan wake
wa viongozi hao kutokana na subira na uvumilivu wao mkubwa na kuongeza
kuwa: Sehemu kubwa sana ya jitihada na kazi muhimu na kubwa zinazofanywa
na viongozi zinafanikishwa kwa subira na uvumilivu wa wake zao ingawa
juhudi hizo za wake wa viongozi mara nyingi huwa hazionekani.
Katika
mkutano huo, Bw. Jahangiri, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya
Kiislamu ya Iran amemshukuru Kiongozi Muadhamu kwa miongozo na nasaha
zake za busara na uungaji mkono wake kwa Serikali na kusema: Serikali
imeandaa ratiba kuu ya kutekeleza kivitendo siasa za uchumi wa
kimuqawama na kwamba siasa hizo ni sawa na cheti cha dawa za kuponya
matatizo ya kiuchumi nchini.
Makamu wa Kwanza wa Rais wa Jamhuri ya
Kiislamu ya Iran ameongeza kuwa: Serikali ina imani na inaziamini
kikamilifu siasa za uchumi wa kimuqawama na kwamba inakubaliana na siasa
hizo kisheria, kikanuni na kiutaalamu.
Bw. Jahangiri amegusia pia
vipaumbele vilivyoainishwa kwa ajili ya uchumi wa Iran katika mwaka huu
wa 1395 Hijria Shamsia katika vikao viwili vya hivi katibuni vya kituo
kikuu cha uchumi wa kimuqawama na kuongeza kuwa: Usiku uliopita
kulifanyika kikao kirefu baina ya Serikali na mashirika makubwa ya
kiuchumi nchini na kwamba Serikali ina nia ya kweli ya kutia nguvu
uzalishaji wa bidhaa za ndani ya nchi, kustawisha usafirishaji nje
bidhaa na kusahilisha ufanyaji kazi, pamoja na kuihusisha vilivyo sekta
binafsi katika ufanikishaji wa mambo hayo.
Amesema, ni jambo la
lazima kwa serikali kusaidiwa na mihimili na taasisi nyingine nchini
hususan Shirika la Sauti na Televisheni la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran
IRIB katika ufanikishaji wa siasa za uchumi wa kimuqawama na kuongeza
kuwa: Ninakuhakikishieni kwamba Serikali haitazembea hata kidogo kutumia
uwezo wake wote wa kielimu, kiuzoefu, uendeshaji mambo na kila uwezo
ilio nao kwa ajili ya kufanikisha siasa za uchumi usioyumba wa
kimuqawama.
Kabla ya mkutano huo, viongozi waliohudhuria mkutano huo
wamesalishwa sala za Adhuhuri na Laasiri na Kiongozi Muadhamu wa
Mapinduzi ya Kiislamu, Ayatullah Udhma Sayyid Ali Khamenei.