Programu hizo zitazinduliwa Masoud Soltanifar Waziri wa Vijana na Michezo Iran na zinajumuisha maonyesho na warsha kuhusu sanaa za Kiislamu na pia kutakuwa na michezo pamoja na tamasha nyiginezo za kiutamaduni.
Mji wa Shiraz katika mwaka wa 2017 utakuwa mwenyeji wa vijana wa nchi za Kiislamu ambao watashiriki katika shughuli zinazohusu mji huo kama mji mkuu wa vijana wa ulimwengu wa Kiislamu.
Kwa zaidi ya miaka 2,000 mji wa Shiraz umekuwa ukitambuliwa kama kitovu cha utamaduni wa Kiajemi au Kifarsi na ni mashuhuri kama kituo cha elimu, ustaarabu na fasihi.
Aidha Shiraz ulikuwa moja ya miji muhimu zaidi ya ulimwengu wa Kiislamu katika zama za kuanzia karne za 9-13 Miladia. Aidha mji wa Shiraz ulikuwa mji mkuu wa Iran katika zama za utawala wa ufalme wa Zand kuanzia mwaka 1747-79 Miladia na ni katika kipindi hicho ndipo majengo yake maridadi zaidi yalijengwa au kukarabatiwa.
Mjini Shiraz pia kuna kaburi au ziara la Shah Cheragh, mwana wa Imam Musa Kadhim AS ambaye ni kati ya Maimamu watoharifu wa Ahlul Bayt (Watu wa Nyumba) wa Mtume Muhammad SAW. Eneo hilo ni moja ya maeneo maarufu ya Ziara kwa Waislamu wa madhehebuya Shia duniani.
Halikadhalika mjini Shiraz kuna makaburi ya Hafez na Saadi, malenga wawili mashuhuri zaidi Wairani. Makaburi hayo yamejengwa kwa usanifu majengo wa kipekee na sawa na maeneo mengine ya Shiraz, yana mabustani ya kuvutia ambayo huwa na mandhari ya kipekee katika msimu wa machipuo. Mji wa Shiraz pia ni mashuhuri kwa misikiti yenye usanifu majengo wa kipekee pamoja na maeneo mengine ya kihistoria.