Ayatullah Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu aliyasema hayo Jumatatu mjini Tehran katika mahafali ya kuwa na ukuruba na Qur'ani Tukufu siku moja kabla ya kuanza Mwezi Mtukufu wa Ramadhani katika ukumbi wa Husseiniya ya Imam Khomeini MA. Kikao hicho cha kila mwaka kilihudhuriwa na idadi kubwa ya wasomaji Qur'ani Tukufu kutoka maeneo yote ya Iran. Akizungumza katika halfa hiyo, Kiongozi Muadhamu amesema, hitajio la leo la kimsingi la wanadamu na jamii za Kiislamu ni kufahamu maarifa ya Qur'ani na kutekeleza mafundisho yake.
Aidha amesisitiza juu ya mafundisho ya Qur'ani Tukufu kuhusu kukabiliana na mustakbirina, makafiri na taghuti.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema moja ya matatizo makubwa katika ulimwengu wa Kiislamu leo ni kutofahamu maarifa ya Qur'ani na kutotekeleza mafundisho ya kitabu hicho kitukufu. Ameongeza kuwa, wale ambao wanalazimisha mataifa kufuata sera za rais au mfalme ni wale wale ambao Qur'ani Tukufu imetoa amri ya wazi ya kukabiliana nao na imesisitiza kuhusu kutowaamini.
Kiongozi Muadhamu ameashiria harakati ya mwamko wa Kiislamu katika baadhi ya nchi katika kipindi cha miaka kadhaa sasa na kusema: "Harakati hii imezimika kutokana na kutoithamini na pia kwa ajili ya kuamini Marekani na utawala wa Kizayuni; lakini Iran, kwa baraka za Imam Khomeini MA, ambaye alikuwa amejawa na maarifa ya Qur'ani iliyathamini mapinduzi yake na tokea siku za awali kabisa hakuyaamini madola makubwa ya kiistikbari bali alisimama kidete kukabiliana nayo.
Katika sehemu nyingine ya hotuba yake, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema Qur'ani Tukufu ni kitabu cha kipekee na kuongeza kuwa: "Kujikurubisha jamii na maarifa ya Qur'ani kutapelekea jamii kuwa imara katika masuala ya dunia na Akhera."