IQNA

Pakistan yalaani kuvunjiwa heshima Qur'ani Tukufu nchini Norway

12:22 - November 25, 2019
Habari ID: 3472230
TEHRAN (IQNA) – Pakistan imelaani vikali hatua ya kuvunjiwa heshima Qur'ani Tukufu na imemkabidhi balozi wa Norway mjini Islamabad malalamiko sambamba na kupanga kuwasilisha malalamiko katika Umoja wa Ulaya na Jumuiya ya Nchi za Kiislamu OIC.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan imemwita balozi wa Norway mjini Islamabad kufuatia maandamano makubwa yaliyofanywa na raia wa Pakistan kulaani kitendo cha kuvunjiwa heshima kitabu cha Mwenyezi Mungu (Qur'an Tukufu) katika moja ya miji ya nchi hiyo ya Ulaya.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Pakistan imetoa taarifa ikisema kuwa mbali na kumwita balozi huyo wa Norway nchini humo imemueleza kwamba kitendo cha kuvunjiwa heshima Qur'an Tukufu kimezijeruhi hisia za Waislamu bilioni moja na milioni 300 duniani ikiwemo nchi ya Pakistan. Taarifa hiyo imeeleza kwamba kitendo hicho kilichofanyika kwa kisingizio cha uhuru wa kujieleza kamwe hakiwezi kuhalalishwa na kwamba Pakistan inaitaka serikali ya Norway kuwachukulia hatua kali wahusika wa kitendo hicho.

Pakistan imebainisha hayo baada ya kundi moja lililo na chuki kubwa dhidi ya Uislamu kwa jina la SIAN huko Norway hivi karibuni kuyavunjia heshima Matukufu ya Kiislamu na Mtume wa Uislamu (SAW) kwa kukichoma moto kitabu hicho cha Mqenyezi Mungu  (Quran Tukufu).

Aidha kamati kuu ya chama cha Tehreek-e-Insaf cha Pakistan chini ya uwenyekiti wa waziri mkuu wa nchi hiyo, Imran Khan imesema itawasilisha kesi hiyo ya kuvunjiwa heshima Qur'ani Tukufu katika Umoja wa Ulaya na Jumuiya ya Ushirikiano wa Nchi za Kiislamu OIC.

3859373

captcha