Ayatullah Ali Khamenei amesema katika ujumbe wake huo: Ninasisitiza kwamba, kuna haja ya kufanyika uchunguzi wa tukio hilo chungu na kuchukuliwa hatua za maana kuhakikisha kwamba, hakujitokezi tena tukio kama hili.
Mwishoni mwa ujumbe wake huo, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amewaombea rehema na maghufira waliopoteza maisha katika mkasa huo wa kuangushwa kimakosa ndege ya abiria ya Ukraine na kuzitakia familia zao subira na ujira mbele ya Mwenyezi Mungu.
Komandi Kuu ya Vikosi vya Ulinzi vya Iran leo Jumamosi imetoa taarifa rasmi na huku ikiashiria vitisho vya rais wa Marekani na majenerali wa kijeshi wa nchi hiyo vya kushambulia maeneo kadhaa muhimu ndani ya ardhi ya Iran sambamba na kuongezeka ndege za kijeshi za magaidi wa Marekani zilizokuwa zinaruka wakati huo karibu na Iran, katika mazingira kama hayo, kulitokea kosa la kibinadamu lililopelekea kutunguliwa ndege hiyo baada ya kukaribia sana katika kituo kimoja nyeti cha kijeshi cha Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu IRGC.
Jumatano asubuhi, ndege moja ya abiria ya shirika la ndege la Ukraine aina ya Boing 737 ilianguka karibu na uwanja wa ndege wa kimataifa wa Imam Khomeini mjini Tehran, ambapo abiria wote 167 pamoja na wahudumu 9 waliokuwemo ndani yake walifariki dunia.
Tukio hilo lilijiri masaa machache baada Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu, IRGC, katika kujibu jinai na ugaidi wa wanajeshi vamizi wa Marekani ambao walimuua shahidi Luteni Jenerali Qassem Soleimani, lilivurumisha makombora ambayo yamelenga kituo cha anga cha jeshi vamizi na la kigaidi la Marekani cha Ain al-Assad nchini Iraq.