IQNA

Palestina yapinga vikali mapatano baina ya UAE, Bahrain na utawala wa Israel

20:28 - September 16, 2020
Habari ID: 3473174
TEHRAN (IQNA) – Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina Mahmoud Abbas amekosoa vikali utiwaji saini wa mapatano ya uanzishwaji uhusiano wa kawaida baina ya Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Bahrain na utawala haramu wa Israel katika ikulu y White House nchini Marekani.

Katika taarifa Abbas amesema amani Mashariki ya Kati itapatikana tu pale utawala wa Israel utakapoondoka katika ardhi za Palestina unaozozikali kwa mabavu sambamba na kutambua haki ya Wapalestina kuwa na nchi ambayo mji mkuu wake utakuwa ni Quds (Jerusalem) Mashariki.

Abbas ametoa taarifa hiyo Jumanne baada ya Rais Donald Trump wa Marekani kushuhudiwa utiwaji saini mapatano kati ya UAE, Bahrain na utawala ghasibu wa Israel.

Makubaliano hayo ya kusaliti malengo matukufu ya Palestina yamelaaniwa na kukosolewa vikali katika Ulimwengu wa Kiislamu.

Wakati huo huo, Bunge la Taifa la Palestina limetangaza kuwa, kufanya mapatano na utawala haramu wa Israel kamwe hakuwezi kuleta amani, utulivu na maendeleo katika eneo la magharibi mwa Asia.

Taarifa iliyotolewa jana usiku na Bunge la Taifa la Palestina imesema kuwa, baada ya kutia saini mapatano ya amani na utawala haramu wa Israel, nchi za Imarati na Bahrain zimeitambua rasmi Quds na matukufu ya Kiislamu na Kikristo ya mji huo kuwa ni mji mkuu wa Israel na kupasisha mpango wa Muamala wa Karne.

Taarifa ya Bunge la Taifa la Palestina imesema kuwa, hatari kubwa na halisi inayotishia usalama wa nchi za Kiarabu na kadhia ya Palestina ni uvamizi wa utawala wa Israel unaofanya mikakati ya kuangamiza kabisa haki za kitaifa za Palestina ikiwa ni pamoja na haki ya kurejea wakimbizi na haki ya kuundwa nchi huru ya Palestina mji wake mkuu ukiwa Quds tukufu. 

3472575

captcha