Fatwa hizo ambazo zimetumwa kwenye ofisi ya Jumuiya ya Kimataifa ya Wanazuoni wa Kiislamu (IUMS) zinajumuisha fatwa na wanazuoni walioshiriki katika kikao cha Jumapili iliyopita cha jumuiya hiyo mjini Doha, Qatar kilichofanyika kwa njia ya video.
Katika fatwa hiyo Jumuiya ya Kimataifa ya Wanazoni wa Kiislamu imesema kuwa: Kinachofanyika baina ya baadhi ya nchi za Kiarabu na Israel si kusitisha vita wala mapato halisi ya amani, bali ni kurudi nyuma na kulegeza kamba mbele ya ardhi tukufu sana na yenye baraka kubwa zaidi ya Kiislamu.
Fatwa ya Jumuiya ya Kimataifa ya Wanazuoni wa Kiislamu imesema kuwa, makubaliano kama hayo yanauhalalisha utawala ghasibu wa Israel, kuutambua rasmi, kubariki mauaji na uhalifu wake mwingine; na masuala haya ni haramu kwa mujibu wa sheria za dini na kanuni za kibinadamu.
Sehemu nyingine ya fatwa hiyo imesema kuwa, hatua kama hiyo inamuwezesha adui mzayuni kutwaa na kughusubu ardhi zaidi ya Palestina.
Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) na utawala wa Kizayuni wa Israel zimefikia makubaliano kuanzisha rasmi uhusiano kamili wa kidiplomasia.
Makubaliano hayo yamekabiliwa na wimbi kali la malalamiko na upinzani wa makundi ya Palestina, nchi za Kiislamu katika eneo la Asia Magharibi na shakhsia wa kisiasa, kijamii na kidini kote duniani.