IQNA

Palestina yasema haitachukua uwenyekiti wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu

17:51 - September 22, 2020
Habari ID: 3473192
TEHRAN (IQNA)- Waziri wa Mambo ya Nje wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina amesema kuwa mamlaka hiyo imeamua kusamehe haki yake ya kuwa mwenyekiti wa Jumuiya ya Nchi za Kiarabu, Arab League.

Riyadh al Maliki ameyasema hayo leo Jumanne lakini wakati huo huo amesema, serikali ya Mamlaka ya Ndani ya Palestina itaendelea kuwa mwanachama wa jumuiya hiyo na haitajitoa licha ya hatua ya baadhi ya nchi za Kiarabu ya kutangaza uhusiano wao wa kawaida na utawala wa Kizayuni, kwani kama itajitoa kutazidi kuzuka pengo katika ulimwengu wa Kiarabu.

Siku kadhaa zilizopita pia, Waziri Mkuu wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina, Mohammad Shtayyeh alisema kuwa, Jumuiya ya Nchi za Kiarabu ndiyo iliyozusha mifarakano na kupoteza mshikamano katika ulimwengu wa Kiarabu.

Hivi karibuni nchi mbili za Kiarabu za Umoja wa Falme za Kiarabu (Imarati) pamoja na Bahrain zilitangaza uhusiano wa kawaida na utawala wa Kizayuni. Usaliti huo umezusha hasira kubwa katika ulimwengu wa Kiislamu na wa Kiarabu. Pamoja na hayo, katika kikao chake cha baada ya matukio hayo, Jumuiya ya Nchi za Kiarabu ilikataa kulaani usaliti huo wa Imarati na Bahrain.

Makundi yote ya Palestina ikiwemo Mamlaka ya Ndani yameungana na wapenda haki duniani kusimama kidete kulaani usaliti wa nchi hizo mbili za Kiarabu na yamekuwa yakisisitiza kuwa yataendelea na muqawama hawadi mwisho.

3924648

captcha