Kwa mujibu wa gazeti la New Vision, msikiti huo mpya ulio katika mji wa Zigoti, wilayani Mityana una nafasi ya waumini zaidi ya 2,000 wakati wa swala. Hivi sasa kuna kampeni ya kuwahimiza Waislamu kupanda miti na maua katika uwanja wa msikiti huo. “Tunataka eneo hili liwe maridadi huku tukilinda mazingira. Miti ya matunda ambayo tunapanda itatupa kivuli na pia itanufaisha vizazi vijavyo,” amesema kiongozi mmoja wa Waislamu katika eneo hilo Ali Kizza.
Amesema pia kuna mpango wa kujenga chuo cha kisasai cha Qur’ani na pia kituo cha tiba kwa ushirikiano na waumini.
Naye Hajji Numan Ntamba, ambaye pia ni mmoja kati ya viongozi wa Waislamu eneo hilo, ametoa wito kwa Waislamu kutumia vizuri msikiti huo kuimarisha imani yao.
Amesema Zigoti ni mji mkubwa wenye Waislamu wengi hivyo wanatakiwa kuutumia msikiti huo ipasavyo. Ameongeza kuwa wanajitahidi kutoa huduma bora kwa Waislamu zikiwemo huduma za afya.
Msikiti huo umejengwa kwa kutegemea michango ya Waislamu wa eneo hilo na pia misaada ya wafadhili nje ya eneo hilo.