Rais Rouhani ameyasema hayo leo Alhamisi wakati wa kufunguliwa Barabara Kuu ya Ghadir na kusema, kukamilika mradi huu pamoja na kuwepo vita vya kiuchumi, vikwazo na mashinikizo ya juu kabisa dhidi ya Iran ni dalili ya wazi ya kufeli adui.
Huku akitoa salamu za pongezi kwa mnasaba wa kukumbuka kuzaliwa Amirul Mumminin Ali AS, Rais Rouhani ameongeza kuwa, kufeli kwa adui kumetokana na subira ya taifa na miongozo ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu.
Hali kadhalika amesema katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita wananchi wa Iran wamesimama kidete mithili ya Imam Ali AS katika kustahamili masaibu.
Rais Rouhani amesema kuzinduliwa Barabara Kuu ya Ghadir ni tukio muhimu sana kwani barabara hii itaunganisha maeneo ya mashariki kuekelea magharibi na magharibi kuelekea kusini mwa nchi. Amesema barabara hiyo ni sehemu ya ile barabara ya kale ambayo ni maarufu kama Barabara ya Hariri.
Barabara Kuu ya Ghadir inapita katika mikoa minne ya Qazvin, Alborz, Markazi na Tehran ambapo mbali na kuchangia katika sekta ya utalii pia itatoa mchango mkubwa katika ustawi wa kiuchumi na usafirishaji mizigo kuelekea nchi jirani.