IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Kukabiliana na vita laini kunahitaji kuwalea vijana wanamapinduzi, wenye azma

21:18 - April 20, 2016
Habari ID: 3470260
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa, ili kukabiliana na vita laini vya kambi ya Uistikbari kuna haja ya kuwandaa na kuwalea vijana wanamapinduzi na wenye azma na irada imara.

Ayatullah Udhma Sayyid Ali Khanei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu aliyasema hayo leo asubuhi aliponana na maelfu ya wajumbe wa Umoja wa Jumuiya za Kiislamu za Wanafunzi kutoka kona zote za Iran na kusema kuwa, moja ya medani muhimu za mapambano baina ya mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu na kambi ya kiistikbari na kibeberu ni suala la vijana. Amesisisitiza kuwa: Kambi inayopambana na mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu inapigania kubadilisha utambiulisho wa kidini na kimapinduzi wa vijana wa Iran na kuwakoponya matumaini, nishati na mori wao, na kwamba njia pekee ya kukabiliana na mashambulio hayo ya siri na tata, ni kulea vijana walioshikamana na dini, wanamapinduzi, wema, wenye misimamo thabiti, wenye mwamko, wenye matumaini na hamasa kubwa, mashujaa na walio tayari kujitolea wakati wote katika njia ya haki na kuwafanya vijana hao kuwa maafisa wa vita laini.
Mwanzoni mwa mkutano huo, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amewausia vijana nchini kutumia vizuri sana fursa hii yenye thamani kubwa ya mwezi wa Rajab na baadae Shaaban na Ramadhani na kusema kuwa: Kipindi cha miezi hii mitatu ni kipindi bora kabisa cha kujijenga kimaanawi na kwamba vijana ambao wako katika kipindi bora na muhimu mno cha umri wao wanaweza kustafidi vizuri sana na fursa hii yenye thamani kubwa kwa ajili ya kujiimarisha kimaanawi.
Baada ya hapo, Ayatullah Udhma Khamenei ametaja baadhi ya medani za mapambano baina ya mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu na kambi ya kiistikbari inayoongozwa na Marekani na Uzayuni na kusema kuwa: Uhuru wa nchi ni pamoja na uhuru wa kisiasa, kiuchumi na kiutamaduni na hiyo ni moja ya medani hizo za mapambano kwani madola ya kibeberu yanakabiliana na nchi yoyote ile inayoamua kusimama kidete kupambana na uistikbari wa mabeberu hao na kulinda uhuru wake.
Aidha amelitaja suala la maendeleo ya nchi kuwa ni medani nyingine ya mapambano baina ya mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu na kambi ya kiistikbari na kusema kuwa: Madola ya kibeberu duniani yanakabiliana na kila nchi ambayo imeamua kujiletea maendeleo yake bila ya kuyategemea madola hayo kwani madola hayo yanatambua vyema kuwa, maendeleo ya namna hiyo huwa funzo na kigezo kizuri kwa mataifa mengine duniani.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu vile vile amesema kuwa, hiyo ndiyo moja ya sababu kuu ya madola ya kiistikbari kusimama na kukabiliana na Iran na kujaribu kulizuia taifa hili kumiliki teknolojia ya nyuklia na kusisitiza kuwa: Kama tutalegeza kamba katika kukabiliana na madola hayo, basi bila ya shaka yoyote upinzani wa madola hayo kwa maendeleo yetu katika nyuga nyingine za bioteknolojia, teknlojia ya Nano pamoja na nyuga nyinginezo za maendeleo utakuwa mkubwa zaidi kwani madola hayo yanapinga maendeleo yoyote yale ya kielimu, kiuchumi na kiustaarabu ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran.
Ayatullah Udhma Khamenei ameitaja nafasi muhimu sana ya Iran katika eneo la magharibi mwa Asia na kushiriki kwake vilivyo katika masuala muhimu duniani, kadhia ya Palestina, suala la muqawama na kadhia ya mtindo wa maisha wa Kiirani-Kiislamu kuwa ni uwanja mwingine wa mapambano baina ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kambi ya kiistikbari. Amesisitiza kuwa: Kama mtindo wa maisha wa Kimagharibi utaeneo katika nchi fulani, basi itakuwa ni jambo rahisi kupenya katikati ya watu muhimu na wenye vipawa wa jamii ya nchi hiyo na kuwazuia kukabiliana na siasa za kibeberu.
Vile vile amezungumzia suala la vijana ambao ni moja ya medani muhimu sana za mapambano baina ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kambi ya kiistikbari na kusema kuwa: Hivi sasa kuna vita vikubwa laini vya chini kwa chini baina ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa upande mmoja na Marekani na Wazayuni kwa upande wa pili kuhusiana na suala la vijana.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema, vijana wanafunzi wa shule za msingi, sekondari na vyuo ndio maafisa wa vita hivyo laini na kuongeza kuwa: Katika vita hivi laini tunaweza kusema kuwa kuna maafisa wa aina mbili wenye utambulisho tofauti na matokeo ya vita hivyo nayo yanaweza kuwa tofauti kulinganana na aina ya maafisa wenyewe.
Ayatullah Udhma Khamenei amesema kuwa, vita laini ni hatari zaidi kuliko vita vya kutumia silaha za kijeshi na kuashiria baadhi ya upayukaji wa maadui na kusema kuwa: Baadhi ya wakati wanatutishia vita vya moja kwa moja vya silaha jambo ambalo ughalati wake umepindukia mipaka kwani hawathubutu hata kidogo kufanya jambo kama hilo na hata tujaalie itokezee wafanye ghalati kama hiyo, basi watakula kipigo wasichokitarajia.
Ameashiria pia namna vita laini dhidi ya mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran vinavyoendelea hivi sasa na ulazima wa taifa la Iran kufikiria pia kushambulia badala ya kujihami tu, na kusisitiza kwamba: Kama katika kambi na ngome ya kivita kutakuwa kuna maafisa walioshikamana vilivyo na dini, wanamapinduzi, wenye misimamo isiyotetereka, wenye mwamko, wachapakazi, wanafikra, mashujaa na walio tayari kujitolea muhanga katika njia ya Mwenyezi Mungu, basi inawezekana kutabiri mapema matokeo ya pambano hilo.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameongeza kuwa: Lakini kama katika kambi na ngome ya vita hivi laini kutakuwa na maafisa walio tayari kusalimu amri, kudanganya na wanaopumbazwa na vicheko na tabasamu za adui, maafisa wasio na mori wala fikra, wasiojali mustakbali wao na wala wa wenzao na wakawa wanashughulishwa tu na starehe na hawaa za nafsi, basi bila ya shaka yoyote matokeo ya vita hivyo nayo yanajulikana.
Ayatullah Udhma Khamenei ameongeza kuwa: Kwa kkuzingatia yote hayo tutaona kuwa, katika vita laini inawezekana kukawa na maafisa wa aina mbili wenye utambulisho na hali tofauti, aina moja ni ya maafisa wanaokubaliwa na Jamhuri ya Kiislamu na aina ya pili ni ya maafisa wanaokubaliwa na kambi ya kiistikbari na aina zote mbili za maafisa hao zinaweza kubadilisha kabisa hatima ya vita hivyo.
Vile vile amesrma kuwa, inaposisitiziwa wajibu wa vijana kushikamana na dini na kuwa wasafi na wacha Mungu na kujiweka mbali na pumbao la kidunia na hawaa za nafsi hakuna maana kabisa ya kufungamanishwa suala hilo na taasubu, fikra mgando na kutoona mbali. Amesema: Wamagharibi na hasa Wamarekkani wanafuatilia kwa karibu kuona vijana wa Iran wanageuka na kuwa watu wasio na imani, wasio mashujaa, wasio na mori na msukumo wowote, wasio na harakati, wasio na matumaini na vile vile wanaowaangalia kwa jicho zuri maadui na wenye mtazamo mbaya na dira na mustakbali wao. Lakini mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu unapigania kujenga na kulea vijana tofauti kabisa na matarajio na ndoto hizo za kambi ya kiistikbari.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu aidha amezitaka kwa kugogoteza jumuiya za Kiislamu za wanafunzi wa shule za msingi, sekondari na vyuo kutilia mkazo suala la kulea vijana wenye muundo na utambulisho wa kidini na kueneza moyo huo kwa vijana wenzao wote wa rika lao na kuongeza kuwa: Kama ambavyo tuna mipango ya muda mrefu ya harakati ya kielimu, kidini na kimapinduzi kwa ajili ya vijana wetu nchini, adui naye ana mipango ya muda mrefu ya kukabiliana na mipango yetu hiyo na kwamba njia pekee ya kukabiliana na kambi hiyo ya maadui ni kuongeza kiwango cha ubora na idadi ya vijana wanamapinduzi nchini walioshikamana vilivyo na dini na wasioyumba wala kutetereka hata kidogo.
Baada ya hapo Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amezungumzia majukumu ya viongozi nchini Iran kuhusu vijana huku akisisitiza kwamba Wizara ya Elimu na Malezi nchini ina watu walioshikamana na dini na inabidi fursa hiyo muhimu, itumike vizuri sana. Amesema, mbali na shule kutoa mafunzo ya kielimu na ya kufundisha madarasani, zinapaswa kuwa na ratiba nyingine sahihi za kuwashirikisha wanafunzi katika kazi za kimapinduzi ili kuhakikisha kuwa kizazi cha vijana kinakuwa ni kizazi cha wanamapinduzi.
Vile vile ameisihi Wizara ya Elimu na Malezi nchini kutoa mwanya na fursa kwa vyama na jumuiya za kimapinduzi kama vile Umoja wa Jumuiya za Kiislamu za Wanafunzi na Basiji ya Wanafunzi na kuongeza kuwa: Kuna habari kwamba baadhi ya shule zinapinga kufanyika kazi za kimapinduzi katika shule hizo, hivyo Wizara ya Elimu na Malezi inapaswa kukabiliana vizuri na jambo hilo.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema pia kuwa, mazingira ya Iran ya kuwa na vijana wengi ni mazingira yanayotia matumaini na kusisitiza kuwa: Pamoja na kuwepo smambo mbali mbali ya upotoshaji na licha ya kuwepo kambi kubwa ya maadui lakini bado nchini Iran kuna vijana waumini, wanamapinduzi, watu wa tawassul, watu wa kutembea masafa marefu kwa miguu wakati wa Arubaini (ya Imam Husain AS), watu wa Qur'ani, watu wa itikafu, watu wenye misimamo imara na watu wanaosimama kidete katika medani za kuyalinda Mapinduzi ya Kiislamu, na inabidi tumshukuru sana Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa neema hiyo.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu pia amesema, kuwepo vijana hao nchini Iran ni jambo adhimu sana na kusisitiza kuwa, baada ya kupita miaka 37 ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu, kambi ya kiistikbari hadi sasa imeshindwa kuiondoa katika uso wa dunia Jamhuri ya Kiislamu ya Iran au kuizuia kustawi na kupata nguvu katika eneo hili na kuongeza kuwa: Pamoja na kuwepo vitisho vikubwa vya kivitendo na kipropaganda vya maadui lakini leo hii Hizbullah ya Lebanon imethibitisha kupevuka kwake katika ulimwengu wa Kiislamu na kwamba kitendo cha serikali fulani fasidi, kibaraka, pumba na isiyo na chochote ndani cha kuilaani harakati hiyo katika kipande fulani cha karatasi; hakina umuhimu wowote ule.
Ayatullah Udhma Khamenei ameashiria pia namna utawala wa Kizayuni wa Israel ulivyokula kipigo kutoka kwa Hizbullah katika vita vya siku 33 na kulinganisha na jinsi jeshi la nchi tatu zenye nguvu za Kiarabu zilivyoshindwa vitani na utawala wa Kizayuni na kusisitiza kuwa: Hizbullah na vijana wake walioshikamana vilivyo na dini wanang'ara mithili ya jua na ni fakhari kwa ulimwengu mzima wa Kiislamu.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu vile vile amesema, dhati ya harakati zinazopigania haki duniani inazidi kuimarikana na kuongeza kuwa: Kuna uwezekano haki ikakumbwa na misukosuko mingi lakini hatima ya yote, haki ndiyo inayoshinda.
Ayatullah Udhma Khamenei ameongeza kuwa, sharti kuu la kuweza kushinda haki ni kusimama imara maafisa wa vita laini katika kukabiliana na matatizo mbali mbali na kusisitiza kuwa: Haki ni ya vijana (wa Iran ambao ni maafisa wa vita laini) na kwa taufiki na uwezo wa Mwenyezi Mungu, kuna siku matatizo yote yataondoka pole pole na vijana wetu watafikia kwenye vilele vya juu vya mafanikio.
Kabla ya hotuba ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, Hujjatul Islam Walmuslimin Hajj Ali Akbari, mwakilishi wa Kiongozi Muadhamu katika Umoja wa Jumuiya za Kiislamu za Wanafunzi ametoa ripoti fupi kuhusu kazi za taasisi hiyo na kusema kuwa: Malengo na shabaha zetu kuu leo hii ni kulea wanafunzi wenye hadhi na daraja inayotakiwa na Mapinduzi ya Kiislamu na ni kwa sababu hiyo ndio maana malezi ya Kimapinduzi kwa kutumia mafundisho ya Kialawi, yakawa ndiyo ajenda kuu ya ratiba na mipango yetu yote.
Vile vile wanafunzi wawili wanachama wa Umoja wa Jumuiya za Kiislamu za Wanafunzi wamepata fursa ya kuzungumza mbele ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu na kutoa mitazamo, madukuduku na daghadagha zao kuhusu kazi na harakati za wanafunzi na masuala ya vijana, masomo na malezi mashuleni.

3490558
captcha