Wamarekani waliosilimu, Bi.Annika Hackfeld na Raymond Martinez
Hakuna shaka kuwa, hivi sasa ni kipindi kigumu kuwa Mwislamu Marekani, lakini kwa waliosilimu wanakumbwa na matatizo na changamoto maradufu ikilinganishwa na waliozaliwa katika familia ya Waislamu.Awali
wengi waliosilumu wanakumbwa na tatizo la upinzani kutoka kwa familia, jamaa na
marafiki ambao huchukizwa na mabadiliko yanayotokea katika maisha ya mwenye
kusilimu. Kwa msingi huo waliosilimu hukumbwa na changamoto kubwa ya kukumbatia
utambulisho wao mpya huku wakiwa chini ya mashinikizo ya pande zote. Katika
upande wa pili waliosilimu nao kama Waislamu wengine pia wanakabiliwa na
changamoto ya chuki dhidi ya Uislamu na Waislamu ambayo imeshadidi katika
kipindi cha utawala wa Donald Trump.
Kwa
mfano, Bi Annika Hackfeld ambaye alilelewa katika familia ya Kikristo na akiwa
na umri wa miaka 18, wakati wa kampeni za uchaguzi wa rais Marekani,
aliikumbatia dini tukufu ya Kiislamu. Katika mahojiano na tovuti ya BuzzFeed, anasema
familia yake ni wafuasi sugu wa Donald Trump na anasema aliwapinga vikali
wakati Trump alipojaribu kutekeleza marufuku ya Waislamu kuingia Marekani mwezi
Januari.
Kwa
upande wake Chris St.Louis anasema aliamua kusoma kuhusu Uislamu baada ya
matukio ya Septemba 11 mwaka 2001. Anasema alipata taufiki ya kuufahamu Uislamu
na akaamua kusilimu na kwamba sasa anahisi utulivu moyoni pamoja na changamoto
alizonazo maishani.
Naye Cassandra
Villareal anasema alilelelwa katiak eneo la kusini mwa Marekani eneo ambalo ni
maarufu kama 'Ukanda wa Bibilia' kutokana na wengi wanaoishi hapo kuwa Wazungu
wenye misimamo mikali ya Kikristo. Villareal anasema kabla ya kusilimu alikuwa
hajwahi kumuona Mwislamu maishani. Anasema uamuzi wake wa kuvaa Hijabu
umepelekea akumbwe na matatizo mengi lakini hajaacha kuvaa vazi hilo la staha
la Kiislamu.
Mfano mwingine ni wa Raymond Martinez ni Mmarekani mwenye asili ya Afrika ambaye anasema aliamua kusilimu baada ya kuhisi amepotea na anahitaji muongozo katika maisha. Anasema baada ya kuanza kutekeleza mafundisho ya Kiislamu maishani, maisha yake yamebadilika na amepata kazi nzuri pamoja na mke anayempenda.
Wote hao wanakabiliwa na changamoto ya kuwa Mwislamu Markeani ambako kunashuhudiwa chuki dhidi ya Uislamu na pia wanakabiliwa na changamoto nyingine ya familia, jamaa na marafiki wanaopinga uamuzi waliochukua wa kuukumbatia Uislamu maishani. Kilichowazi ni kuwa, kuenezwa chuki dhidi ya Uislamu na Waislamu kumepelekea idadi kubwa ya wasiokuwa Waislamu Marekani na nchi zingine duniani kupata hamu ya kuujua Uislamu ambapo wengi wanaopata taufiki hatimaye husilimu baada ya kuutambua ukweli. Taasisi ya Marekani ya PEW katika uchunguzi wake uliochapishwa Mei mwaka huu ilitangaza kuwa Uislamu ndio dini inayoenea kwa kasi zaidi duniani.