IQNA

Kiongozi Muadhamu

Kuwa imara taifa la Iran kumeighadhabisha Marekani na kuivutia dunia

17:32 - January 20, 2020
Habari ID: 3472390
TEHRAN (IQNA) - Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amefafanua kuhusu misingi ya fikra za Kiislamu na malengo yake kukiwemo kusimama imara kwa Jamhuri ya Kiislamu na kusema hiyo ni nukta inayoivutia dunia.

Ameongeza kuwa, sababu ya kuwafanya Wamarekani wachukizwe na kughadhabishwa na taifa la Iran ni mvuto unaotokana na fikra ya kusimama imara mfumo wa kujitegemea mkabala wa utawala wa kidhalimu.

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ameyasema hayo leo mjini Tehran alipokutana na viongozi wanaosimamia ibada ya Hija ambapo amesisitiza juu ya fursa za ibada ya Hija kwa ajili ya kufikisha ujumbe mpya wa Jamhuri ya Kiislamu kwa walimwengu, kama kiigizo chema cha serikali ya kidemokrasia ya kidini. Ameongeza kwamba, kiigizo chema cha demokrasia ya kidini kwa ajili ya walimwengu bado hakijafahamika vyema mkabala wa mamilioni ya nyenzo za kipropaganda ambazo hii leo zinaenezwa dhidi ya Iran, na kwamba ibada hii tukufu ya Hija inaweza kuwa fursa nzuri kwa ajili ya kubainisha kiigizo hicho chema na masuala mengine kama vile sababu ya uadui wa Marekani dhidi ya Iran na mantiki ya taifa la Iran kutokubali kuburuzwa na madola makubwa ya kibeberu.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu sambamba na kusisitizia umuhimu wa suala la ibada ya Hijja kama moja ya harakati za kisiasa, kiitikadi na kijamii ameongeza kwamba, hata hivyo nchi nyingi duniani zimeghafilika na umuhimu wa taathira ya ibada hiyo. Amesema, pamoja na hayo Hijja ni nukta muhimu ya kufanyika harakati ya kimataifa yenye maslahi mengi kwa umma wa Kiislamu.

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ameashiria juhudi mbalimbali za madola ya kibeberu duniani kwa ajili ya kuzuia umoja wa umma wa Kiislamu na kusema kuwa, umma wa Kiislamu ambao maana yake halisi ni kuwa kitu kimoja na irada na malengo ya pamoja bado haujaundwa na kwamba jambo la kusikitisha ni kuona wito wa kutakakuwepo umoja wa Kiislamu ukikabiliwa na kila aina ya tuhuma, dharau na kuenezwa vita katika nchi za Kiislamu. Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema kuwa makusudio ya Wamarekani kwamba eti ni lazima Iran iwe nchi ya kawaida, ni kuitaka Jamhuri ya Kiislamu ya Iran iwache kuwasilisha fikra mpya duniani (ambayo ni kunufaika na fikra za wananchi na za mafundisho ya Kiislamu katika kuendesha nchi)  na kuongeza kuwa kubainishwa misingi ya kisiasa ya mfumo wa Jamhuri ya Kiislamu pamoja na kuwafahamisha walimwengu fikra zake mpya ni sehemu nyingine ya majukumu muhimu na ya lazima katika ibada ya Hija.

3872952

captcha