IQNA

AMIRI JESHI MKUU WA IRAN

Ni lazima tuwe na nguvu ili vita visiibuke na adui asitishe vitisho

19:05 - February 08, 2020
Habari ID: 3472451
TEHRAN (IQNA) - Amiri Jeshi Mkuu wa vikosi vya ulinzi vya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema, kuna ulazima wa Iran kuwa na nguvu katika pande zote hasa katika uga wa ulinzi; na akasisitiza kwamba: "Ni lazima kuwa na nguvu ili vita visiibuke na vitisho viishe."

Ayatullah Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu na Amiri Jeshi Mkuu wa vikosi vyote vya ulinzi katika Jamhuri ya Kiislamu ya Irna, ametoa sisitizo hilo leo mjini Tehran katika mkutano wa kila mwaka na makamanda na wafanyakazi wa kikosi cha anga na kikosi cha ulinzi wa anga cha jeshi la Iran.
Ameashiria kwamba, kuwa dhaifu kunamtia hamasa adui ya kuchukua hatua; na akaongeza kuwa: "Sisi hatuna dhamira ya kutoa kitisho kwa nchi na taifa lolote lile, bali tunataka kulinda usalama wa nchi na kuzuia vitisho."
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ameviasa vikosi vya ulinzi vya Iran vifanye jitihada za kuimarisha miundomsingi ya ulinzi katika pande zote, viwe na umakini katika utendaji wa kazi muhimu na kutumia kikamilifu vipawa na uwezo uliopo. Amesema: Kama marais waliopita wa Marekani walikuwa wakitumia visingizio mbalimbali kutekelezea ushetani wa utawala huo, leo hii upotofu, uwashaji moto wa vita, uzushaji fitna na uchu wa Marekani kwa mali za mataifa mengine unafanyika waziwazi na bila kificho; lakini hakuna shaka yoyote, njia hiyo batili inayofuatwa na maadui wa taifa la Iran itagonga mwamba tu.
Ayatullah Khamenei ameashiria pia vikwazo vya Marekani dhidi ya Iran na akabainisha kuwa: Vitisho vitageuzwa kuwa fursa, na vikwazo ambavyo ni hatua ya kihalifu, vinaweza kuwa sababu ya kuiokoa nchi na utegemezi wa mafuta na ya utatuzi wa matatizo mengi.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ametanabahisha kwa kusema: Bila shaka baadhi ya watu werevu ndani ya utawala wa Marekani wameshaling'amua jambo hili na wamesema, tusiruhusu Iran iwe na uchumi usiotegemea mafuta, kwa sababu hiyo, inapasa tufungue njia ili uchumi wa Iran usijivue kikamilifu na utegemezi wa mafuta; kwa hiyo viongozi na hasa na wanaohusika na uchumi inapasa wawe macho na suala hili.
Aidha ameashiria jinsi nyenzo na mbinu wanazotumia maadui zilivyo tata zaidi hivi sasa na akasisitiza kwa kusema, njia na mbinu inazotumia Jamhuri ya Kiislamu katika kukabiliana na hayo, nazo pia zimekuwa tata zaidi kuliko ilivyokuwa huko nyuma, kiasi kwamba zimeweza kupindua hila za adui.

3877246

captcha