IQNA

Msikiti wahujumiwa Ulm, Ujerumani, uchunguzi waanza

12:22 - February 10, 2020
Habari ID: 3472456
TEHRAN (IQNA) – Watu wasiojulikana wameuhujumu msikiti katika mji wa Ulm nchini Ujerumani katika tukio linalohesabiwa kuwa ni la chuki dhidi ya Uislamu.

Kwa mujibu wa taarifa, watu wasiojulikana pia wameuhujumu chumba kinachotumiwa na Waislamu kusali katika mji huo ulio katika jimbo la Baden-Württemberg kusini mwa Ujerumani.

Msemaji wa polisi mjini Ulm, Wolfgang Jurgens anasema hujuma  hizo zilijiri usiku katika siku za 27,28, na 31 mwezi uliopita wa Januari na kusababisha hasara ya Euro 4,000.

Jurgens anasema hakuna ushahidi hadi sasa wenye kuthibitisha kuwa hujuma hizo zimetekelezwa kwa malengo ya kisiasa au kidini.

Hujuma dhidi ya maeneo hayo ya ibada ya Waislamu zimelaani na Baraza la Dini mjini Ulma ambalo limesema  kuna uhuru wa kuabudu Ujerumani ambao ni haki ya binaadamu inayolindwa na katiba ya nchi hiyo. Baraza hilo ambalo linawaleta pamoja wafuasi wa dini mbali mbali limetangaza kufungamana na Waislamu na kutoa wito kwa wakazi wa mji huo kuwa macho na kushirikiana ili wafuasi wa dini zote  waishi pamoja kwa maelewano.

Ujerumani imeshuhudia ongezeko la chuki dhidi ya Waislamu na wahamiaji katika miaka ya hivi karibuni, chuki ambazo zinachochewa na vyama vya mrengo wa kulia vyenye misimamo ya kuvurutu ada dhidi ya watu wasiokuwa Wajerumani asili.

Ujerumani ni nchi yenye idadi ya watu zaidi ya milioni 81 na ina Waislamu takribani milioni tano na hivyo kuifanya nchi ya pili kwa idadi ya Waislamu Ulaya Magharibi baada ya Ufaransa.

3470594

captcha