IQNA

Nasaha za Kiongozi Muadhamu kuhusu kukabiliana na kirusi cha Corona

16:54 - March 03, 2020
Habari ID: 3472527
TEHRAN (IQNA) - Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ametoa maelekezo muhimu kuhusiana na mradhi yaliyoenea ya COVID-19 yanayosababishwa na kirusi cha corona humu nchini Iran.

Katika mnasaba wa Siku ya Miti na Wiki ya Maliasili, Ayatullah Sayyid Ali Khamenei sambamba na kupanda miche miwili ya matunda amesema kuwa upandaji miti ni harakati yenye baraka za Mwenyezi Mungu.

Akizungumzia suala la kuenea kwa kirusi cha Corona nchini Iran amesema: "Kama ambavyo hapo kabla niliwashukuru kwa dhati madaktari, wauguzi na wahudumu katika sekta ya afya, kwa mara nyingine ni lazima niwapongeze tena shakhsia hawa wanaofanya kazi kubwa katika jihadi ya kumtumikia Mwenyezi Mungu." Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu sambamba na kuomba dua ya kupona wagonjwa wote na pia kuwaombea rehma na msamaha watu waliofariki dunia ameongeza kwa kusema: "Haifai tuzembee kuhusu usia na maelekezo ya viongozi kuhusiana na njia za kuzuia kuenea kwa maradhi haya, kwa kuwa Mwenyezi Mungu ametutaka kujihisi ni wenye majukumu kuhusiana na afya zetu na za watu wengine."

Kadhalika Kiongozi Muadhamu ametoa usia kwa watu wote kufanya wasila na kumuomba dua Mwenyezi Mungu na kusema: "Sitaki kuidunisha balaa hii, hata hivyo balaa hili sio kubwa kama inavyokuzwa na kumewahi kujiri balaa kubwa zaidi ya hii. Mimi nina matumaini kuhusu dua za vijana na wacha-Mungu wenye mioyo safi katika kuomba kuondolewa mabalaa makubwa kwa kuwa kufanya wasila mbele za Mwenyezi Mungu na kuomba shufaa kwa Mtume Mtukufu wa Uislamu na Maimamu watoharifu kunaweza kuondoa matatizo mengi."

Aidha ameashiria suala la nchi nyingi za dunia kukumbwa na kirusi cha Corona na kusema: "Tangu siku ya kwanza viongozi wetu walitangaza suala hili kwa uwazi na ukweli mwingi na kuwaweka wazi wananchi, hata hivyo baadhi ya nchi ambazo maradhi haya yameenea sana na kusambaa zinaficha, hata hivyo sisi tunamuomba Mwenyezi Mungu atupe afya njema." Amezungumzia hatua nzuri na za kuvutia za baadhi ya wananchi wa Iran za kujitolea kifedha na kugawa suhula na zana za kitiba na kusema, matendo hayo mazuri na kwa kuzingatiwa mafanikio haya, balaa na vitisho vinaweza kubadilika na kuwa fursa nzuri na amesema kuwa ana matumaini siku za afya kamili ya wananchi wa Iran zinakaribia.

3882908

captcha