IQNA

Wanamgambo wa Haftar washambulia msikiti nchini Libya

11:18 - April 27, 2020
Habari ID: 3472708
TEHRAN (IQNA) – Wanamgambo wa jenerali muasi Khalifa Haftar nchini Libya wameushambulia msikiti karibu na mji mkuu wa nchi hiyo, Tripoli.

Kwa mujibu wa taarifa msikiti uliolengwa uko katika mji wa Ain Zara, kusini mwa Tripili. Taarifa ya Serikali ya Muafaka wa Taifa Libya (GNA) inayoongozwa na Waziri Mkuu Faez al-Sarraj imesema msikiti huo umeharibiwa vibya baada ya kuvurumishiwa makombora kadhaa.

Tarehe 4 Aprili 2019, kundi la Khalifa Haftar lilianzisha mashambulizi makali dhidi ya mji mkuu wa Libya Tripoli kwa tamaa ya kuuteka mji huo na kuipindua Serikali ya Mwafaka wa Kitaifa inayotambuliwa kimataifa. Hata hivyo ndoto hiyo haijatimia hadi leo hii.

Baada ya kupinduliwa utawala wa Muammar Gaddafi huko Libya mwaka 2011, nchi hiyo ilitumbukia katika vita vya ndani na hivi sasa kuna serikali mbili hasimu, moja ya mashariki na nyingine ya magharibi mwa nchi hiyo ambapo vikosi vya pande hizo mbili vinaendelea kupigana.

Serikali hizo mbili hasimu ziliibuka mwaka 2014 ambapo moja ina makao makuu yake mjini Tobruk, mashariki mwa nchi na inaungwa mkono na Jenerali muasi Khalifa Haftar, na nyingine ni Serikali ya Muafaka wa Kitaifa Libya (GNA) inayoongozwa na Waziri Mkuu Fayez al-Sarraj ambayo inatambuliwa rasmi na Umoja wa Mataifa na ambayo inasimamia maeneo ya magharibi mwa nchi hiyo ukiwemo mji mkuu, Tripoli. Haftar anapata uungaji mkono wa nchi kama vile Misri, Imarati na Saudi Arabia ambazo zinataka kuipuindua serikali ya al-Sarraj inayotambuliwa na Umoja wa Mataifa na inayoonekana kuungwa mkono na Uturuki.

3894465

captcha