IQNA

Mamlaka ya Ndani Palestina yasifu EU kwa kulaani vurugu za Israel Ukingo wa Magharibi

19:13 - November 28, 2025
Habari ID: 3481581
IQNA – Makamu wa Rais wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina, Hussein al-Sheikh, amesifu tamko la pamoja la Ufaransa, Ujerumani, Italia na Uingereza lililolaani kuongezeka kwa mashambulizi ya utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi.

Al-Sheikh, akizungumza Alhamisi, alisema Mamlaka ya Palestina inathamini msimamo huo wa mawaziri wa mambo ya nje wa mataifa hayo, akilitaja kuwa “hatua muhimu” ya kulinda raia na kusitisha mashambulizi. Pia alisisitiza haja ya kuunga mkono juhudi za kimataifa za kufanikisha suluhisho la mataifa mawili na kuimarisha amani na uthabiti.

Kwa mujibu wa takwimu za Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuratibu Misaada ya Kibinadamu (UNOCHA), walowezi wakoloni wa Kizayuni walitekeleza mashambulizi 264 dhidi ya Wapalestina mwezi Oktoba pekee ikiwa idadi kubwa zaidi tangu shirika hilo lianze kurekodi matukio hayo mwaka 2006.

Katika tamko lao, mawaziri wa Ulaya walisema: “Tunalaani vikali kuongezeka kwa vurugu za Israel dhidi ya Wapalestina katika Ukingo wa Magharibi. Tunaitaka Israel kutekeleza wajibu wake chini ya sheria za kimataifa na kuwalinda Wapalestina. Ni lazima iwawajibishe wahusika na kuzuia mashambulizi zaidi.”

Aidha, mawaziri hao walionyesha wasiwasi kuhusu kuidhinishwa kwa zaidi ya vitengo 3,000 vya makazi haramu katika wiki tatu zilizopita chini ya mpango wa E1, unaolenga kupanua Ma’ale Adumim,  moja ya makazi makubwa zaidi ya Kizayuni yaliyojengwa kwenye ardhi ya Palestina. Walihimiza Israel kuachana na sera hiyo.

3495543

captcha