Meja Jenerali Hossein Salami ametoa kauli hiyo leo Jumatano katika Kongamano la Mashahidi 92 elfu wa Jeshi la Basiji hapa Tehran na kusema, katika fitna za hivi karibuni za maadui wa taifa la Iran, madola ya kiistikbari yalitaka kutumia fitna hizo kufidia vipigo vya mara kwa mara yanavyopata kutoka kwa taifa la Iran lakini wameshindwa.
Ameongeza kwa kusema: Maadui walitaka kuunganisha fitna hiyo na mashinikizo yao ya kiwango cha juu zaidi dhidi ya Iran lakini wananchi wa taifa hili la Kiislamu walikuwa macho na kufelisha kikamilifu njama zao hizo.
Kamanda Mkuu wa Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu aidha ametoa onyo kali kwa maadui akiwaambia wasivuke mistari myekundu ya Iran. Amesisitiza kuwa, iwapo adui atafanya chokochoko zozote zile, basi taifa la Iran litamuangamiza huko huko aliko.
Meja Jenerali Salami aidha amesema, taifa la Iran limeweza kusimama imara katika kulinda matukufu yake ya kitaifa na Kiislamu kwa zaidi ya miaka 40 sasa na kuongeza kuwa, Iran inaendelea mbele na njia yake kwa nguvu na umakini wa hali ya juu na karibuni hivi itakuwa dola kubwa duniani.
Akiashiria shari ya Marekani duniani, Kamanda Mkuu wa IRGC amesema, Marekani haitaki chochote katika mataifa ya dunia isipokuwa umasikini, kubakia nyuma kimaendeleo, uporojai utajiri wa nchi, uwe ni wa kimaada au kimaanawi.