IQNA

Kiongozi Muadhamu: Mwaka mpya ni wa uzalishaji, uwezeshaji na uondoaji mikwamo na vizuizi

19:49 - March 20, 2021
Habari ID: 3473750
TEHRAN (IQNA)- Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ametoa ujumbe maalumu kwa mnasaba wa kuingia leo mwaka wa Kiirani wa 1400 wa Hijria Shamsia na mbali na kutoa mkono wa baraka za mwaka huo mpya wa Nairuzi amesema: Mwa huu ni wa uzalishaji, uwezeshaji na uondoaji mikwamo na vizuizi.

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ametoa mkono wa baraka na fanaka wananchi wenzake wote hasa familia za mashahidi, majeruhi wa vita na mataifa yote yanayoadhimisha sikukuu ya Nowruza au Nairuzi kwa mnasaba huo na kumuomba Mwenyezi Mungu awatilie baraka za kimaada na kimaanawi akisema kuwa, mwaka huu wa 1400 Hijria Shamsia umesadifiana na sikukuu za mwezi wa Shaabani ikiwemo sikukuu ya Nusu ya Shaaban na kuzaliwa Imam wa Zama, Imam Mahdi AS ikiwa ni ishara ya baraka nyingi za mwaka huu.

Amesema, mwaka ulioisha wa 1399 Hijria Shamsia ulijaa matukio ya kila namna na ya mara ya kwanza kutokea hususan maradhi yasiyojulikana na COVID-19. Amesema ugonjwa huo wa corona umetoa pigo kubwa kwa watu wote ikiwemo sekta ya kazi na ajira, sekta ya elimu, mikusanyiko ya kidini, michezo, safari na ziara na kadhalika.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu pia amesema, ni jambo zito sana kuona makumi ya maelfu ya wananchi wamekufa kutokana na COVID-19 na hilo ndilo tukio chungu zaidi la mwaka ulioisha wa 1399 Hijria Shamsia. Amewaombea rehema na maghufira ya Mwenyezi Mungu wananchi wote waliotangaulia mbele ya Haki kwa ugonjwa huo na kuzipa mkono wa pole familia zao.

Ayatullah Sayyid Ali Khamenei amezungumzia pia jinsi taifa la Iran lilivyovifelisha vikwazo vya kiwango cha juu zaidi vya adui akisema kwamba, maadui wa Iran wakiongozwa na Marekani walikusudia kulipigisha magoti taifa la Iran. Amesema: Tab'an sisi tulikuwa tunajua kwamba taifa leo litasimama kidete kujihami na maadui watashindwa tu, lakini leo hii Wamarekani wenyewe na marafiki zao wa Ulaya wanakiri waziwazi kuwa vikwazo vya kiwango cha juu zaidi dhidi ya taifa la Iran, vimeshindwa.

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amegusia pia uchaguzi muhimu wa rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran unaotarajiwa kufanyika baadaye mwaka huu na kuahidi kulizungumzia kwa upana zaidi jambo hilo katika hotuba yake ya kila mwaka ya Nowruz.

3960726

captcha