IQNA

Rais Rouhani: Maadui wamesambaratika baada ya Wairani kusimama kidete

20:13 - March 20, 2021
Habari ID: 3473751
TEHRAN (IQNA)- Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema leo katika ujumbe maalumu kwa mnasaba wa kuwadia mwaka mpya wa Kiirani wa 1400 Hijria Shamisa kwamba kusimama imara taifa la Iran kumepelekea kushindwa maadui.

Rais Hassan Souhani ametoa mkono wa baraka kwa mnasaba wa kuingia leo mwaka mpya wa Kiirani wa 1400 Hijria Shamsia na kugusia vita vya kidhulma na vya kikatili vya kiuchumi vilivyoanzishwa na adui dhidi ya taifa la Iran na kusema kuwa, taifa la Iran liliingia katika vita dhidi ya ugonjwa wa COVID-19 katika hali ambayo lilikuwa linanyimwa hata msaada wa chini kabisa wa kupambana na ugonjwa huo hatari. Si hayo tu, lakini Iran ilikuwa imewekewa vikwazo na benki za dunia, vya hata kupata fedha zake za kuiwezesha kupambana na janga hilo. 

Rais Rouhani amesema, kipindi hicho kigumu sana, na mtihani huo mkubwa na vita vya wakati mmoja wa pande tofauti havikulipigisha magoti taifa la Iran, bali kimekuwa ni kipindi cha kung'ara na kupata fakhari kubwa taifa hili katika historia yake.

Amesema, leo hii maadui wa Iran wanakiri kwamba hawawezi kuzungumza na taifa hili kubwa kwa lugha ya vitisho, ubabe na vikwazo kwani baada ya kupita miaka mitatu, sasa hivi wamelazimika kurudi katika njia ya kuamiliana kwa njia za busara na taifa imara la Iran.

Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameongeza kuwa, katika upande wa siasa za kimataifa pia, taifa la Iran limepata mafanikio makubwa ya mfululizo katika Umoja wa Mataifa, Baraza la Usalama na Mahakama ya Kimataifa ya Jinai ICC kiasi kwamba leo hii, Iran ina mawasiliano mapana, ya kina na ya kiistratijia na dunia huku maadui wa taifa hili wakizidi kutengwa katika misimamo yao dhidi ya Iran.

Vile vile amewahimiza wananchi wa Iran kujitokeza kwa wingi katika uchaguzi wa rais unaotarajiwa kufanyika mwaka huu humu nchini na kusema kuwa, kushiriki kwa wingi na kwa hamasa kubwa katika uchaguzi, ni utangulizi na ndilo sharti la lazima la kufanikishwa malengo ya taifa la Iran katika muongo wa kwanza wa karne hii ya 15 ya mwaka wa Kiirani wa Hijria Shamsia.

Tarehe Mosi Farvardin inayosadifiana na Machi 20 au 21 huwa siku ya kwanza ya mwaka wa Kiirani ya Hijria Shamsiya. Siku hii ambayo ni mwanzo wa msimu maridadi wa machipuo hapa nchini ni maarufu kwa jina la Sikukuu ya Nowruz au Nairuzi kwa lugha ya Kiswahili. Nowruz ni moja kati ya sherehe za kale zaidi duniani na ilianza kusherehekewa zaidi ya miaka 3000 iliyopita. Mbali na Iran nchi ambazo husherehekea Nowruz ni pamoja na Afghanistan, Jamhuri ya Azerbaijan, Albania, Kyrgyzstan, Turkmenistan, Macedonia, India, Uturuki, Jamhuri ya Tatarstan nchini Russia, Sudan na Zanzibar nchini Tanzania. Mwaka 2010 Umoja wa Mataifa ulitangaza rasmi tarehe Mosi Farvardin yaani 21 Machi kila mwaka kuwa ni Siku ya Kimataifa ya Nowruz. Umoja wa Mataifa umeitambua Siku ya Nowruz kama siku kuu ya kale ambayo huadhimishwa wakati wa kuwadia msimu wa machipuo na kuhuishwa tena mazingira.

3960748

Kishikizo: rouhani iran nowruz
captcha