Mkurugenzi wa zamani wa kitengo cha taarifa potovu katika mtandao wa Facebook, Frances Haugen amefichua nyaraka za namna ambavyo shirika hilo limekuwa likikabiliana na mijadala katika mtandao huo wa kijamii katika kipindi cha miaka saba.
Amesema Facebook imekuwa ikiunga mkono taarifa za kueneza hofu na dhidi ya ubinadamu ambazo zinafungamana na jumuiya moja yenye misimamo mikali ya kitaifa na Kihindu India inayojulikana kama Rashtriya Swayamsevak Sangh (RSS), ambayo inaonekana kuwa ni kitengo cha idiolojia cha chama tawala cha Bharatiya Janata (BJP).
Aidha amesema Facebook ilikuwa inaweka rekodi cha taarifa za kichochezo na chuki dhidi ya Waislamu India lakini ilikataa kuchukua hatua.
India ina watumizi milioni 530 wa Facebook na hivyo kuifanya kuwa soko kubwa zaidi la mtandao huo wa kijamii.
Kwa muda mrefu sasa chama tawala India cha BJP, chenye misimamo mikali ya Kihindu, kimekuwa kikitekeleza kampeni ya makusudi dhidi ya Waislamu wa eneo la Assam ambao ni zaidi ya asilimia 33 ya wakazi wa jimbo hilo la kaskazini mashariki.
Mwaka 2018, serikali ya Waziri Mkuu Narendra Modi iliwapokonya uraia mamilioni ya Waislamu wa Assam kwa madai kuwa ni wahajiri haramu kutoka nchi jirani ya Bangladesh.
Kuanzia Septemba 20 oparesheni ya kuwatimua Waislamu kutoka nyumba zao imeanza na hadi sasa familia 800 zimelazimishwa kuondoka.