Shirika la Habari la Saudia (SPA) limeandika kuwa: "Kwa ushirikiano na Mamlaka ya Data na Akili za Kubuni au Artificial Intelligence Saudia (SDAIA), Wizara ya Hija na Umrah inatangaza kuzinduliwa huduma mpya ambayo itawawezesha wale walio nje ya nchi kupata vibali vya Umrah na Sala katika Msikiti Mtakatifu wa Makka na pia kuzuru Msikiti wa Mtume SAW kwa kujisajili kupitia Aplikesheni za 'Eastmarna' na 'Tawakkalna'.
Wizara hiyo imesema aplikesheni hizo zitaweza kutumika punde baada ya wageni wanaoingia nchini humo kujisajili katika tovuti ya "Quddum" ambayo ni maalumu kwa wale wanaowasili Saudia.
Wizara ya Hija na Umrah Saudia imewataka wafanyaziara wote kuhakikisha kuwa wana nakala mpya ya aplikesheni za Eatmarna na Tawakkalna katika simu zao za mkononi.
Mwezi uliopita, Wizara ya Hija na Umrah Saudia ilitangaza kuwa wale wote wenye nia ya kutekeleza ibada ya Umrah hawatahitajika tena kusubiri siku 14 kama ilivyokuwa hapo kabla kutokana na janga la COVID-19.
Oktoba 16 Wizara ya Mambo ya Ndani ya Saudia ilitangaza kupunguza vizuizi ambavyo vilikuwa vimewekwa katika ufalme huo ili kuzuia maambukizi wa COVID-19. Kwa mujibu wa kanuni mpya ni ruhusha waumini kujaa kama kawaida katika Msikiti Mtakatifu wa Makka na Msikiti wa Mtume SAW mjini Madina.