Walinzi wanasema walimuona mtu akimwaga petroli katika Msikiti Mkuu wa Cologne lakini akatatoroka alipogundua kuwa ameshaonekana. Mshukiwa huyo aliacha baiskeli yake, mtungi wa petroli na vibiriti wakati akitoroka. Polisi wametoa wito kwa mashahidi wa tukio hilo wajitokeze na kwamba watatumia kamera kujaribu kumnasa mshukiwa huyo.
Msikiti huo ni mashuhuri zaidi mjini Cologne unasimamiwa na na Jumuiya ya Kiislamu-Kituriki ya Masuala ya Kidini (DITIB) na kwa mara kadhaa sasa umepokea barua za vitisho kutoka kwa watu wenye misimamo mikali ya kibaguzi wanaopinga Uislamu na makundi ya Wanazi-Mamboleo.
Ujerumani ni nchi yenye watu milioni 82 na inakadiriwa kuwa Waislamu ni takribani asilimia 6.7 nchini humo.
Katika miaka yahivi karibuni kumeshuhudiwa ongezeko la hujuma dhidi ya Waislamu na misikiti Ujerumani kutokana na kukithiriwa fikra za chuki dhidi ya Uislamu.