IQNA

Ufaransa yapiga marufuku Hijabu katika michezo

15:39 - January 20, 2022
Habari ID: 3474830
TEHRAN (IQNA)- Baraza la Seneti la Ufaransa limepiga kura na kuidhnisha sheria inayopiga marufuku wanawake Waislamu kuvaa vazi la stara na heshima la Hijabu katika mashindano ya michezo.

Hatua hiyo ambayo ni muendelezo wa chuki dhidi ya Uislamu inatarajiwa kuzusha makelele na malalamiko mengi wakati mji mkuu wa Ufaransa Paris unatarajiwa kuwa mwenyeji wa mashindano ya Olimpiki mwaka 2024.

Maseneta 160 walipiga kura ya ndio kuunga mkono marufuku hiyo huku wenzao 143 wakipinga.

Hata hivyo haijafahamika kama marufuku hiyo itajumuisha mashindano ya michezo ya Olimpiki hapo mwaka 2024 au la.

Wajuzi wa mambo wanasema kuwa, endapo marufuku hiyo itajumuisha mashindano ya kimataifa ya michezo ya Olimpiki itakayofanyika mjini Parsi mwaka 2024 huenda mashindano hayo yakakabiliwa na changamoto kubwa.

Hii ni kutokana na kuwa, kama wanamichezo Waislamu watasusia mashindano hayo itakuwa pigo kubwa hasa kwa kuzingatia kuwa, katika mashindano ya Olimpiki ya Tokyo 2020 wanamichezo Waislamu walikuwa na nafasi na hisa kubwa ya medali katika mashindano hayo.

Shirikisho la Mpira wa Miguu la Ufaransa huko nyuma limewahi kuchukua hatua za chuki dhidi ya Uislamu ambapo lilikuwa likiwakataza wanawake Waislamu kuvaa kitambaa cha kichwa katika mashindano rasmi ya michezo.

Huko nyuma pia Baraza la Seneti la Ufaransa limewahi kupasisha mpango unaopiga marufuku wasichana wenye umri chini ya miaka 18 kuvaa Hijabu katika maeneo ya umma.

Tangu Rais Emmanuel Macron aliposhika hatamu za uongozi nchini Ufaransa, vitendo vya chuki dhidi ya Uislamu na hata kuvunjiwa heshima matukufu ya  Uislamu vimeongezeka mno katika nchi hiyo ya bara Ulaya.

Hivi karibuni  kamati maalumu ya Bunge la Kitaifa la Ufaransa iliidhinisha sheria ya 'thamani za jamhuri' ambazo zilipendekezwa na rais Emmanuel Macron wa nchi hiyo kwa ajili ya kukabiliana na kile alichokitaja ni 'Uislamu wa wanaotaka kujitenga.'

Waziri wa Mambo ya Ndani Ufaransa amedai katika ukurasa wake wa Twitter kuwa sheria hiyo inalenga kulinda thamani za jamhuri sasa na siku za usoni.

Katika miezi ya hivi karibuni Ufaransa imeshadidisha mbinyo dhidi ya Waislamu nchini humo ambapo hata maduka ya Waislamu yanafungwa kwa visingizio mbali mbali.

Maafisa wa serikali za mitaa Ufaransa sasa wanatumia kila kisingizio kufunga biashara za Waislamu ikiwa ni katika kutekeleza sera jumla za Rais Emmanuel Macron ambaye ameanzimia kuwadhoofisha Waislamu nchini humo.

Ufaransa ina idadi kubwa zaidi ya Waislamu barani Ulaya. Kwa mujibu wa takwimu za mwaka 2016, kuna zaidi ya Waislamu milioni 5.7 Ufaransa ambao ni takribani asilimia 8.8 ya watu wote nchini humo.

4030029

captcha