IQNA

Mashindano ya Qur'ani

Qari wa Comoro asema ndoto yake imetimia katika Mashindano ya Kimataifa ya Qur'ani ya Iran

14:44 - February 22, 2024
Habari ID: 3478396
IQNA - Qari wa Qur'ani Tukufu kutoka Visiwa vya Comoro (Komoro) amesema ndoto yake imetimia kwa kupata fursa ya kushiriki katika Mashindano ya Kimataifa ya Qur'ani Tukufu ya Iran.

Abdul Rahman Ahmad Hafiz ameiwakilisha nchi yake katika Awamu ya 40 ya Mashindano ya Kimataifa ya Qur'ani ya Iran yaliyomalizika Jumatano mjini Tehran.

Katika mahojiano na Shirika la Habari za Qur'ani la Kimataifa (IQNA), amesema tangu zamani alikuwa na ndoto ya kushiriki katika tukio hilo adhimu la Qur'ani na hatimaye akapewa fursa hiyo mwaka huu.

Abdul Rahman alisema alianza mafunzo ya Qur'ani akiwa na umri mdogo katika nchi yake na kisha akaendelea kuboresha ujuzi wake wa Qur'ani nchini Kenya.

Alibainisha kwamba wazazi wake wote wawili ni wahifadhi wa Qur'ani Tukufu

Nchini Comoro, ambako takriban watu wote ni Waislamu, watu wana shauku kubwa ya kujifunza Quran na kuna idadi kbya ya waliohifadhi Qur'ani, hasa miongoni mwa wanawake na wasichana, alisema.

Akiwa nchini Kenya, alijifunza usomaji wa Qur'ani  kwa Hafs kupitia mtindo wa Asim na aliweza kupokea idhini ya kuwa qari.

Abdul Rahman pia alibainisha kwamba mwalimu wake wa kwanza wa Qur'ani katika  mbinu Maqamat na Naghamat alikuwa Muirani aitwaye Saeed Rahimi, ambaye kwa sasa anaishi Madagaska.

Ama kuhusu maqari waliomvutia na ambavyo anawaiga amesema anapande usomaji wa Qur'an wa marehemu Sheikh Muhammad Rif’at wa Misri na maqari Wairani Saeed Rahimi wa Iran na Seyed Javad Hosseini.

Aidha ameitaja Jamhuri ya Kiislamu ya Iran  kuwa ni taifa la Qur'ani na kusema anajivunia kupata fursa ya kuhudhuria mashindano hayo nchini Iran.

Fainali ya Awamu ya 40 ya Mashindano ya kimataifa ya Qur'ani ya Iran  ilizinduliwa mjini Tehran siku ya  17 Februari na inamalizika Jumatano Februari 21.

Rais wa Iran, Sayyid Ebrahim Raisi alishiriki katika sherehe za kufunga mashindano na iliyofanyika jijini Tehran ambapo mbali na kuhutubu aliwakabidhi washindi zawadi.

Jumla ya wahifadhi na wasomaji 69 kutoka nchi 44 wanashindana katika fainali katika kategoria kuu za usomaji wa Qur'ani (kwa wanaume) na kuhifadhi Qur'ani na usomaji wa Tarteel (kwa wanaume na wanawake).

Hafla hiyo ya kila mwaka, inayoandaliwa Shirika la Iran la Wakfu na Misaada, inalenga kukuza utamaduni na maadili ya Qur'ani miongoni mwa Waislamu na kuonyesha vipaji vya wasomaji na wahifadhi Qur'ani.

4200994

Habari zinazohusiana
captcha