"Kwa nini wakati watu wa dini zingine wanapotenda jinai, hatuoni dini yaoi ikinasibishwa na uhalifu wautendao,?" amehoji Sheikh Abdallah Kheri, mhadhiri wa Kiislamu katika chuo kikuu cha umma nchini Kenya katika mahojiano na tovuti ya OnIslam.net.
'Hivi karibuni mhubiri kanisani alipatikana na mada za kutengeneza mabomu Kenya lakini vyombo vya habari havikumtaja kama Mkristo mshukiwa wa ugaidi. Undumakuwili huu unapaswa kukomeshwa," ameongeza.
Wasi wasi wa Sheikh Kheir na Waislamu kwa ujumla umetokana na ripoti ya hivi karibuni ya halmashauri inayoratibu vyombo vya habari Kenya ambayo ilikosoa vyombo vya habari Kenya kuwa vinawaonea Waislamu wakati wa kutangaza habari kuhusu ugaidi.
Ripoti ya Baraza la Vyombo vya Habari Kenya iliyokuwa na anuani ya: "Tathmini Kuhusu Ugaidi: Nafasi ya Vyombo vya Habari Kenya katika Kuibua Chuku za Kidini na Misimamo Mikali" ilifikia natija kuwa vyombo vya habari Kenya kwa kawaida huwataja Waislamu kama magaidi au walio na uwezo wa kuwa magaidi.
Ripoti hiyo ilihoji ni kwa nini vyombo vya habari Kenya hutumia maneno au istilahi ambazo zinahusisha vitendo vya ugaidi na Uislamu au Waislamu.
Ripoti hiyo imesema kutumiwa maneno kama vile "Ugaidi wa Kiislamu", "Uislamu Wenye Misimamo Mikali", 'Wanaharakati wa Kiislamu" na "Waislamu Wenye Misimamo Mikali" wakati wa kutangaza habari kuhusu ugaidi ni jambo ambalo hupelekea kuongezeka chuki dhidi ya Uislamu kutokana na kuunasibisha ugaidi na uhalifu na Uislamu au Waislamu.
Ripoti hiyo pia imesema kuwa vita baina ya serikali ya Kenya na magaidi wa Al Shabab hutajwa kimakosa kuwa ni vita vya kidini baina ya Wakristo na Waislamu na hivyo kuchochea zaidi uhasama wa kidini na kikabila katika nchi hiyo ya mashariki mwa Afrika.