IQNA

Ayatullah Araki atoa wito kwa Waislamu wawe macho kuhusu njama za maadui

22:10 - January 09, 2015
Habari ID: 2689576
Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kimataifa ya Kukurubisha Madhehebu ya Kiislamu amewataka Waislamu kuwa macho katika kukabiliana na njama za maadui wa ulimwengu wa Kiislamu.

Akihutubu kabla ya sala ya Ijumaa iliyosaliwa leo  mjini Tehran, Ayatullah Muhsin Araki amebainisha njama za maadui wa umma wa Kiislamu za kuzusha fitina na mifarakano baina ya  Waislamu na kusisitiza kwamba, maadui wanaelewa wazi  kwamba, iwapo Waislamu watashikamana na kuwa kitu kimoja, kuna uwezekano wa kuwa na nguvu kubwa zaidi  ulimwengu katika siku zijazo. Ayatullah Araki ameongeza kuwa, maadui kwa kutumia Ushia na Usuni wanachochea hitilafu na mifarakano katika nchi za Iraq, Syria, Yemen na katika maeneo mengine ya ulimwengu wa Kiislamu ili waweze kuzuia kuundwa umma mmoja wa Kiislamu wenye nguvu kubwa duniani. Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kimataifa ya Kukurubisha Madhehebu ya Kiislamu ameelezea baadhi ya hitilafu za kimitazamo zilizoko baina ya Masuni na Mashia na kusisitiza kuwa, makundi hayo yote mawili ni ya Kiislamu  na yanaamini  kuwepo Mwenyezi Mungu mmoja,  utume wa Nabii Muhammad (saw), Qurani Tukufu na Kibla kimoja. Ayatullah Araki ameongeza kuwa, uadui na chuki kubwa za  serikali za Marekani, Uingereza na utawala wa Kizayuni wa Israel dhidi ya Jamhuri ya Kiislamu ya Iran zinatokana na misaada na uungaji mkono wa taifa la Iran kwa wananchi madhulumu wa Palestina.../mh

2688540

captcha