Taarifa zinasema kuwa, shambulio hilo la makombora mawili lilifanyika Jumapili katika eneo la mashamba ya Amal yaliyoko katika eneo la kiistratijia la Quneitra lililoko umbali wa kilomita 60 kusini mwa Damascus, mji mkuu wa Syria. Harakati ya Hizbullah imethibitisha kuuawa wanachama wake sita kwenye shambulio hilo, akiwemo Abu Issa mmoja wa makamanda na mtaalamu wa operesheni za vita wa Hizbullah na Jihad Mughniya mtoto wa shahidi Emad Mughniya Kamanda wa zamani wa Hizbullah. Taarifa ya Hizbullah imeeleza kuwa, shambulio hilo limefanyika wakati wanachama hao walipokwenda kukagua eneo la mashamba ya Amal. Duru za habari zinasema kuwa, gari iliyowabeba wanachama hao wa Hizbullah imeteketezwa kabisa, na nyingine kuharibiwa vibaya. Ndege za Israel zimekuwa zikishambulia mara kwa mara maeneo ya Syria tokea zilipoanza ghasia na machafuko nchini humo yapata miaka minne iliyopita. Takwimu zilizotolewa na Umoja wa Mataifa zinaonyesha kuwa, hadi sasa watu wasiopungua laki mbili wameshauawa kwenye vita vya ndani nchini Syria.../mh