Ayatullah Sayyed Ali Khamenei, Kiongozi wa Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu
ameyasema hayo leo mjini Tehran kwa mnasaba wa sherehe ya siku ya kuzaliwa Bibi
Fatima Zahraa SA binti wa Mtume Muhammad SAW alipokutana na wasomaji
wa tungo za kumsifu Mtume na Ahlu Baiti wake AS. Amesisitizia pia umuhimu wa kuelewa nafasi chanya ya mwanamke wa Kiislamu.
Kiongozi Muadhamu amesema kuna
uwezekano mkubwa kwamba kumfanya mwanamke kuwa chombo cha anasa katika
ulimwengu wa Magharibi, ni sehemu ya njama za Wazayuni kwa ajili ya
kusambaratisha jamii ya mwanadamu.
Sambamba na kubainisha sababu ya kuenezwa nara za kama ile ya 'uadilifu
na usawa wa kijinsia' katika nchi za Magharibi, amesema kuwa uadilifu ni
kutambua vipawa na tunu alizopewa na Mwenyezi Mungu kuzistawisha.
Kiongozi Muadhamu amesema kuwa, hii leo wasomi wa Magharibi na watu
wanaonadi usawa wa kijinsia wanajutia hatua yao hiyo kutokana na makosa
mengi yanayosababishwa na suala hilo. Vilevile ameashiria sira na
harakati adhimu ya Bibi Fatima Zahraa AS, mwanamke mtukufu wa Kiislamu
katika nafasi ya kiongozi halisi na wakati huo huo kama mke na mama wa
aina yake na kumtaja kuwa ni kiigizo chema na kamili kwa ajili ya
Waislamu.'
Itakumbukwa kuwa, siku kama ya leo miaka 1446 iliyopita yaani sawa na tarehe 20 Jamadu
th-Thani mwaka wa nane kabla ya Hijiria, alizaliwa Bibi Fatima Zahraa
SA Binti ya Mtukufu Mtume Muhammad SAW. Tangu utotoni mwake, Bibi
Fatima alikulia katika nyumba ya wahyi na chini ya malezi bora ya baba
yake Nabii wa Allah na hivyo kufikia daraja la juu la ukamilifu katika
elimu na ubora. Aidha Bibi Fatimah SA alikuwa na nafasi muhimu katika
kupunguza machungu na tabu zilizokuwa zikimkumba baba yake katika
harakati za kueneza mafundisho ya dini ya Uislamu, kutoka kwa
washirikina.
Mwaka wa pili Hijiria binti huyo mtukufu wa Mtume alifunga
ndoa kwa sherehe nyepesi sana na Imamu Ali Bin Abi Twalib, ambaye naye
ni dhihirisho la haki, uadilifu na uchaji-Mungu. Akiwa na Imamu Ali SA Bibi Fatimah aliishi kwa Amani na furaha ya juu huku akitekeleza
majukumu ya mke na mama mwema kwa watoto wake watukufu, yaani Imamu
Hassan AS, Imamu Hussein AS na Bibi Zainab SA.