Zahid Hafeez Chaudhry amesema Pakistan inalaani vikali hatua ya hivi karibuni ya kuchomwa moto Qurani Tukufu katika mji wa Malmo nchini Sweden na Oslo huko Norway na kueleza bayana kuwa: Kuongezeka kwa vitendo vya chuki dhidi ya Uislamu (Islamophobia) kunaenda kinyume kabisa na moyo na mafundisho ya dini yoyote ile.
Ameongeza kuwa, kuheshimu matukufu, imani na mafundisho ya dini nyinginezo ni wajibu wa pamoja na jambo la dharura kwa ajili ya amani na ustawi duniani.
Hivi karibuni, watu wenye chuki dhidi ya Uislamu na Waislamu walifanya maandamano katika mji mkuu wa Norway, Oslo huku mmoja wao akionekana akichana kurasa za Qurani Tukufu na kuzitemea mate.
Aidha Ijumaa iliyopita, wafuasi wa mwanasiasa Rasmus Paludan, ambaye anaongoza chama cha chenye misimamo mikali cha mrengo wa kulia ambacho kinapinga Waislamu huko nchini Sweden, walijumuika kinyume cha sheria mjini Malmo na kukivunjia heshima Kitabu Kitukufu cha Waislamu.