IQNA

Maandamano Iran kulaani kuvunjiwa heshima Mtume Muhammad SAW

14:56 - September 10, 2020
Habari ID: 3473156
TEHRAN (IQNA) - Wananchi wa Iran wanaendelea kufanya maandamano katika maeneo mbali mbali kupinga hatua ya kuvunjia heshima Mtume Muhammad SAW nchini Ufaransa.

Katika mji wa Qum, ulio kusini mwa Tehran, wakazi na wanafunzi wa vyuo vya mji wa Qum wamefanya maandamano makubwa wakilaani hatua ya jarida la Kifaransa la Charlie Hebdo ya kumvunjia heshima Mtume Muhammad SAW.

Waandamanaji hao walikusanyika katika Haram Takatifu ya Bibi Maasouma (SA) wameukosoa Umoja wa Mataifa kwa kutochukua hatua ya maana ya kukabiliana na hujuma na utovu wa adabu wa jarida hilo la Ufaransa la kumvunjia heshima Mtume Muhammad (saw) na matukufu ya Kiislamu.

Vilevile Ofisi ya Taasisi ya Kulingania Uislamu ya Qum imetoa taarifa ikilaani kitendo cha jarida la Kifaransa la Charlie Hebdo cha kuchapisha vibonzo ninavyomkebehi na kumvunjia heshima Mtume wa mwisho wa Mwenyezi na kusema kuwa, hatua hiyo ni kielelezo cha kuporomoka ubinadamu na ustaarabu wa Wamagharibi.

Jumatano iliyopita, kwa mara nyingine tena jarida la Kifaransa la Charlie Hebdo liliamua kwa makusudi kuwafanyia kejeli na istihzai Waislamu na dini tukufu ya Uislamu kwa kuchapisha vibonzo vinavyomvunjia heshima Mtume Muhammad SAW.

Hivi karibuni pia watu wenye chuki dhidi ya Uislamu walichoma moto na kuteketeza nakala ya Qur'ani katika mji wa Malmo nchini Sweden. 

Vitendo hivyo vya chuki dhidi ya Uislamu na Waislamu vimeendelea kulaaniwa na wapenda haki, watu huru na wenye dhamira safi kote ulimwenguni hususan katika Ulimwengu wa Kiislamu. 

84033818

captcha