IQNA

Rais wa Palestina amshukuru Ayatullah Sistani kwa kuitetea Palestina

20:50 - March 14, 2021
Habari ID: 3473733
TEHRAN (IQNA)- Rais Mahmoud Abbas wa Mamlaka ya Ndani ya Palestina amemwandikia barua Ayatullah Ali Sistani kiongozi wa juu wa kidini wa Waislamu wa madhehebu ya Shia nchini Iraq kumpongeza na kumshukuru kwa misimamo yake ya kuitetea na kuihami Palestina katika mkutano wake na Papa Francis, Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani.

Katika barua yake hiyo, Mahmoud Abbas ametoa mkono wa heri na baraka kwa mnasaba wa Idi ya Mab'ath ya kupewa Utume Bwana Mtume Muhammad SAW na akaeleza kwamba taifa la Palestina linauthamini uungaji mkono wa Ayatullah Sistani kwa suala la Palestina na mapambano ya Wapalestina ya kupigania haki zao ikiwemo ya kujitawala na kuwa taifa huru.

Jumamosi ya wiki iliyopita, Kiongozi wa Kanisa Katoliki Duniani Papa Francis alifika katika mji wa Najaful-Ashraf nchini Iraq ambapo alikutana na kufanya mazungumzo ya faragha ya muda wa saa moja na Ayatullah Sistani, Marjaa Taqlidi wa Waislamu wa madhehebu ya Shia nchini humo.

Kwa mujibu wa taarifa ya ofisi ya Ayatullah Sistani, katika mazungumzo na Papa Francis, kiongozi huyo wa juu wa kidini nchini Iraq alizungumzia changamoto kubwa zinazoikabili jamii ya wanadamu katika zama hizi ikiwemo kutokuwepo kwa uadilifu, umasikini, maudhi na unyanyasaji wa kidini na kifikra na ukandamizaji wa uhuru wa msingi wa watu na akabainisha kuwa, watu wengi duniani na hasa wananchi wa Palestina wanateseka kutokana na dhulma, ufakiri, kukosa uhuru wa msingi, uadilifu wa kijamii, vita na mzingiro wa kiuchumi.

Ayatullah Sistani aliongeza kuwa viongozi wa kidini na kimaanawi wanapaswa kutimiza wajibu wao ili kupunguza machungu na mateso hayo; na kwa pande zinazohusika kutumia mantiki na hekima katika mienendo yao.

3959369

 

captcha