IQNA

Viongozi wa dunia waipongeza Iran katika maadhimisho ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu

17:06 - February 12, 2022
Habari ID: 3474920
TEHRAN (IQNA)- Wakuu wa nchi mbalimbali walituma ujumbe wa kuipongeza Jamhuri ya Kiislamu ya Iran kwa mwaka wa 43 wa ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu.

Miongoni mwa waliotuma jumbe zao ni waziri mkuu wa Armenia na marais wa Senegal, Ivory Coast, Kyrgyzstan, Tajikistan, Belarus Jamhuri ya Azerbaijan na wengine wengi.

Rais wa Senegal ametoa mkono wa baraka na fanaka kwa serikali na taifa la Iran kwa mnasaba wa kuadhimisha mwaka wa 43 wa ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu.

Balozi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran mjini Dakar, Mohammad Reza Dehshiri, ameandika katika mtandao wa kijamii wa Twitter kwamba, Rais Macky Sall wa Senegal amemtumia ujumbe Rais Ebrahim Raisi wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kutoa mkono wa baraka kwa serikali na taifa la Iran kwa mnasaba wa kuadhimisha mwaka wa 43 wa ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu nchini Iran.

Katika ujumbe wake huo, Rais Sall amesema kuwa, uhusiano wa nchi yake na Iran ni wa kuridhisha na kwamba Dakar iko tayari kuimarisha zaidi na zaidi uhusiano wake na Jamhuri ya Kislamu katika nyuga na sekta zote.

Katika ujumbe wake kwa Rais wa Iran Ebrahim Raeisi, Waziri Mkuu wa Armenia Nikol Pashinyan ameupongeza uongozi na wananchi wa Iran kwa mnasaba huo na kusisitiza kukuza uhusiano kati ya nchi hizo mbili kwa msingi wa kuaminiana na kuheshimiana.

Rais wa Kyrgyzstan Sadyr Japarov katika ujumbe wake alitoa wito wa kuendelezwa kwa ushirikiano na Iran, jambo ambalo litapelekea kuimarika kwa uhusiano kati ya mataifa hayo mawili rafiki.

Alisema Bishkek itatumia utaratibu wote wa ushirikiano wa pande mbili na wa kimataifa ili kuimarisha uhusiano na Tehran.

Emomali Rahmon, rais wa Tajikistan, alikuwa kiongozi mwingine aliyempongeza rais na watu wa Iran katika hafla hiyo.

Alisema Dushanbe ina nia ya kupanua uhusiano wake wa pande mbili na Tehran katika nyanja tofauti.

Rais wa Belarus Alexander Lukashenko katika salamu zake za pongezi aliashiria uhusiano mkubwa kati ya Iran na Belarus na kuashiria uwezo mkubwa wa kuimarisha zaidi uhusiano huo.

Ujumbe mwingine uliotumwa kwa Rais Raeisi ulikuwa kutoka kwa Ilham Aliyev, mwenzake kutoka Jamhuri ya Azerbaijan.

Kiongozi huyo wa Azeri alisema uhusiano wa nchi hizo mbili unatokana na matakwa ya mataifa hayo mawili ambayo yameishi katika mazingira ya kirafiki na yana maadili sawa.

Vile vile amepongeza uhusiano unaoongezeka kati ya Tehran na Baku na kusema ziara za maelewano za maafisa wa Iran na Azeri zitapelekea kuimarika zaidi uhusiano huo.

Kila mwaka, mamilioni ya Wairani kote nchini huadhimisha siku kumi za kuadhimisha kumbukumbu ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu ya mwaka 1979 yaliyokomesha utawala wa kifalme wa utawala wa Pahlavi unaoungwa mkono na Marekani nchini humo.

Siku ya kurejea kwa Imam Khomeini nchini Iran (Februari 1 mwaka huu) ni mwanzo wa Siku Kumi za Fajr (alfajiri), ambazo zinafikia kilele kwa mikusanyiko ya maadhimisho ya ushindi wa Mapinduzi ya Kiislamu tarehe 11 Februari.

Taifa la Iran liliupindua utawala wa Pahlavi ulioungwa mkono na Marekani miaka 43 iliyopita, na hivyo kuhitimisha miaka 2,500 ya utawala wa kifalme nchini Iran

Mapinduzi ya Kiislamu yaliyoongozwa na hayati Imam Khomeini-Mwenyezi Mungu Amrehemu- yalianzisha mfumo mpya wa kisiasa unaozingatia maadili na demokrasia ya Kiislamu.

/4035673

captcha