IQNA

Jinai za Israel

Jeshi katili la Israel lamuua shahidi kijana Mpalestina

16:05 - June 29, 2022
Habari ID: 3475443
TEHRAN (IQNA)- Wanajeshi wa utawala katili wa Israel wamempiga risasi na kumuua kijana wa Kipalestina walipokuwa wakivamia sehemu ya kaskazini ya Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan huku hali ya wasiwasi ikiongezeka katika maeneo yanayokaliwa kwa mabavu na utawala huo katika wiki za hivi karibuni.

Maafisa wa matibabu walimtambua mwanamume huyo wa Kipalestina aliyeuawa shahidi kuwa Mohammad Maher Marei aliyekuwa na umri wa miaka 23.

Walisema Marei, mkazi wa kambi ya wakimbizi ya Jenin, alifariki kutokana na majeraha mabaya aliyoyapata wakati wa makabiliano na wanajeshi wa Israel wakati wanajeshi hao walipovamia kitongoji cha mashariki cha Jenin Jumatano asubuhi.

Duru za ndani zimeongeza kuwa kijana mwingine wa Kipalestina, ambaye utambulisho wake haukujulikana mara moja, pia alijeruhiwa wakati wa uvamizi huo.

Vikosi vya Israel pia vimewakamata vijana wawili wa Kipalestina, waliotambulika kwa jina la Yahya Yousef al-Jafar na Ahmed Asaad Nabhan, baada ya kuvamia nyumba za jamaa zao katika kitongoji cha al-Marah mashariki mwa Jenin.

Shirika la habari la Shehab la Palestina limeripoti kuwa, mamia ya Wapalestina waliandamana katika vitongoji vya Jenin na kambi yake ya wakimbizi baada ya uvamizi huo wakiwa wamebeba maiti ya mwenzao aliyeuawa shahidi wakipiga nara dhidi ya Israel, kulaani jinai za utawala huo ghasibu unaotenda jinai kila uchao dhidi ya Wapalestina.

Vile vile wametoa wito wa kuwepo mapambano makali ya ukombozi kamili wa maeneo yote ya Wapalestina yanayokaliwa kwa mabavu na utawala wa Israel.

Wakati huo huo, wanajeshi wa Israel wamemtia mbaroni kijana mmoja katika Mji Mkongwe wa al-Quds (Jerusalem) unaokaliwa kwa mabavu kutokana na madai ya kuwachoma visu maafisa wa utawala huo ghasibu.

Polisi walifunga lango la kuingilia katika eneo la Msikiti wa al-Aqsa na maeneo mengine ya Mji Mkongwe mara baada ya mshukiwa ambaye jina lake halikutajwa, mkazi wa mji wa Beit Lahm ( Bethlehem) wa Ukingo wa Magharibi wa Mto Jordan, kukimbia baada ya kudaiwa kujaribu kuwachoma kisu polisi  wa utawala katili wa Israel Jumanne usiku.

Kulingana na polisi wa Israel, hakuna maafisa waliojeruhiwa katika shambulio hilo linalodaiwa kutekelezwa.

3479510

captcha