Mwaka mpya wa Kiirani wa 1402 Hijria Shamsia ulianza Machi 21 na idadi kubwa ya wananchi katika Jamhuri ya Kiislamu ya Iran huukaribisha mwaka mpya kwa kufika katika maeneo ya kiibada hasa Haram Takatifu ya Imam Ridha AS katika mji mtakatifu wa Mashhad.
Hujjatul Isalma Hujjat Gonabadinejad, naibu wa kitamaduni, kijamii na ziara wa gavana wa jimbo la Khorasan Razavi, alisema mashirika tofauti ikiwa ni pamoja na Manispaa ya Mashhad, kamati ya usafirishaji, na Wizara ya Barabara na Maendeleo ya Miji imefanya maandalizi ya kutoa huduma wafanyaziara.
Ameongeza kuwa kutokana na kuwasili kwa mwezi mtukufu wa Ramadhani, wafanyaziari wengi wanatarajiwa kurejea katika miji yao baada ya kuzuru madhabahu tukufu ya Imam Ridha AS.
Mapema mwezi huu, Mohsen Davari, gavana wa Mashhad, alisema kuwa makao makuu yameanzishwa ili kuratibu juhudi za kuwahudumia wafanyaziara.
Aliongeza kuwa wafanyaziara wote watakaribishwa katika sehemu za kuingilia iwe wanasafiri kwa nchi kavu, kwa ndege au kwa gari moshi.
Afisa huyo aliongeza kuwa usimamizi wa hoteli na kituo cha malazi umeimarishwa ili kuhakikisha wanatoa huduma zinazostahiki.
Mashhad ni makao ya kaburi la Imam Ridha AS, Imam wa 8 wa Waislamu wa madhehebu ya Shia. Ni moja ya vivutio vya kidini vilivyotembelewa zaidi ulimwenguni.
Makumi ya mamilioni ya wafanyaziara kutoka Iran na nchi nyingine hutembelea mji huo mtakatifu kila mwaka.
Ni mojawapo ya maeneo yanayopendwa sana na Wairani wakati wa likizo ya Nowruz ambayo inaashiria mwanzo wa Mwaka Mpya wa Kiirani au Kiajemi.
4129477