IQNA

Qur'ani Tukufu Inasemaje /50

Umuhimu wa umoja miongoni mwa Waumini

17:29 - May 09, 2023
Habari ID: 3476979
TEHRAN (IQNA) – Tofauti za mitazamo wakati mwingine zinaweza kusababisha migawanyiko miongoni mwa waumini wa dini tukufu ya Kiislamu. Lakini Qur'ani Tukufu inapendekeza njia maalum ya kukabiliana nia mifarakani na inawaalika wote kwenye umoja.

Mwenyezi Mungu anasema katika Aya ya 103 ya Surah Al Imran: “Na shikamaneni kwa Kamba ya Mwenyezi Mungu nyote pamoja, wala msifarikiane. Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo juu yenu: vile mlivyo kuwa nyinyi kwa nyinyi maadui naye akaziunganisha nyoyo zenu; kwa neema yake mkawa ndugu. Na mlikuwa ukingoni mwa shimo la Moto, naye akakuokoeni nalo. Namna hivi Mwenyezi Mungu anakubainishieni Ishara zake ili mpate kuongoka".

Maana ya aya ya “kamba ya Mwenyezi Mungu” ni kila fikra inayotuunganisha na Mwenyezi Mungu yaani Uislamu, Qur'ani Tukufu, Mtukufu Mtume Muhammad (SAW) na Ahl-ul-Bayt wake au watu wa nyumba yake (AS).

Aya hii inaashiria neema kubwa ya umoja na udugu na inawataka Waislamu kutafakari juu ya hali ya kusikitisha ya huko nyuma na kulinganisha mifarakano iliyotangulia na umoja uliopatikana

Aidha ayah ii inaashiria kuzikurubisha nyoyo za waumini kwa Mwenyezi Mungu, na kusema: “Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo juu yenu: vile mlivyo kuwa nyinyi kwa nyinyi maadui naye akaziunganisha nyoyo zenu; kwa neema yake mkawa ndugu. Hii inaweza kutajwa kama moja ya miujiza ya Uislamu ambayo ilieneza urafiki miongoni mwa Waarabu wakati walipokuwa katika uhasama na vita kabla ya ujio wa Uislamu.

Mambo Muhimu kutoka katika Aya ya 103 ya Surah Al Imran

Kuunda umoja kati ya mioyo inawezekana tu kwa taufiki yake Mwenyezi Mungu. Katika Aya ya 63 ya Surah Al-Anfal, Mwenyezi Mungu anamwambia Mtukufu Mtume (SAW): “… Na akaziunga nyoyo zao. Na lau wewe ungeli toa vyote viliomo duniani usingeli weza kuziunga nyoyo zao, lakini Mwenyezi Mungu ndiye aliye waunganisha. Hakika Yeye ndiye Mtukufu Mwenye nguvu na Mwenye hikima.”

Mfarakano na migawanyiko ni miongoni mwa adhabu za Mwenyezi Mungu. Nukta nyingine ni kuwa katika Uislamu kutosema ukweli kwa madhumuni ya kuleta umoja inajuzu na kusema ukweli unaoweza kusababisha mfarakano ni Haramu.

Nukta muhimu tunazojifunza:

  1. Umoja na kuepuka mifarakano ni kazi ya Mwenyezi Mungu kwa watu. “Na shikamaneni kwa Kamba ya Mwenyezi Mungu nyote pamoja …”
  2. Msingi wa umoja uwe ni dini ya Mwenyezi Mungu, si rangi, lugha, utaifa n.k. “Na shikamaneni kwa Kamba ya Mwenyezi Mungu nyote pamoja …”
  3. Mtu asisahau baraka na huduma za Uislamu. “Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo juu yenu. ; kwa neema yake mkawa ndugu.
  4. Umoja ni sababu ya udugu. “… kwa neema yake mkawa ndugu.”
  5. Umoja ni miongoni mwa neema kubwa za Mwenyezi Mungu. “… kwa neema yake mkawa ndugu.”
  6. Mfarakano na mifarakano ni mashimo ya moto. " Na mlikuwa ukingoni mwa shimo la Moto, naye akakuokoeni nalo."
  7. Neema za Mwenyezi Mungu ni Ishara zake. “Namna hivi Mwenyezi Mungu anakubainishieni Ishara zake ili mpate kuongoka.”
  8. Kukumbuka neema za Mwenyezi Mungu kunatayarisha njia ya uongofu. “Na kumbukeni neema ya Mwenyezi Mungu iliyo juu yenu: vile mlivyo kuwa nyinyi kwa nyinyi maadui naye akaziunganisha nyoyo zenu.”
captcha