IQNA

Kaaba Tukufu yasafishwa katika tukio la kila mwaka

11:00 - July 11, 2025
Habari ID: 3480928
IQNA – Msikiti Mtukufu wa Makka uliangaziwa na tukio la kipekee Alhamisi, ambapo shughuli ya kila mwaka ya kuosha Kaaba (Ghusl ya Kaaba) ilitekelezwa kwa heshima na taadhima kubwa.

Hafla hiyo, iliyojaa uzito wa kiroho na historia ya muda mrefu, iliongozwa na Naibu Mkuu wa Mkoa wa Makka, Mwanamfalme Saud bin Meshal, akiongozana na maulamaa, maafisa wa ngazi za juu wa Saudia na wageni mashuhuri kutoka ulimwengu wa Kiislamu.

Katika hafla hiyo adhimu, eneo la ndani ya Kaaba lilisafishwa kwa kutumia mchanganyiko wa maji ya Zamzam, maji ya waridi, na marashi ya oud ya hali ya juu. Pia, ukuta wa ndani wa Kaaba ulipakwa manukato, kwa utaratibu wa kipekee unaolenga kuonyesha heshima ya hali ya juu kwa Nyumba ya Mwenyezi Mungu ambayo ni Kibla cha mabilioni ya Waislamu kote duniani.

Hafla  hiyo ya Ghusl hufanyika mara mbili kila mwaka  kabla ya mwezi mtukufu wa Ramadhani, na tena katika mwezi wa Muharram baada ya ibada ya Hija. Ingawa ni watu wachache waliobahatika kushiriki moja kwa moja, picha na video za tukio hilo huenezwa kote duniani, na hivyo kuwawezesha Waislamu wengi kushiriki kiroho katika tukio hilo tukufu.

3493787

Kishikizo: kaaba makka
captcha