IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Udharura wa kutumiwa sanaa ya mashairi kuwaongoza walengwa

21:22 - July 02, 2015
Habari ID: 3322405
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesisitiza juu ya udharura wa kutumiwa vyema sanaa ya mashairi kwa ajili ya kutoa miongozo kwa walengwa.

Ayatullah Udhma Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Mualdhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ya Iran ameyasema hayo Jumatano mjini Tehran alipokutana na majimui ya wataalamu wa utamaduni, wahadhiri wa mashairi na fasihi ya Kifarsi, washairi vijana na magwiji wa tungo za kishairi wa Iran pamoja na washairi kadhaa kutoka nchi za India, Pakistan, Afghanistan, Tajikistan na Azerbaijan.  Kikao hicho kimefanyika katika usiku wa kuamkia siku ya kuzaliwa "Karimu Ahlul Bayt" Imam Hasan al Mujtaba Alayhis Salaam.
Katika mkutano huo, Ayatullah Udhma Khamenei ametoa mkono wa baraka na fanaka kwa mnasaba wa kukumbuka siku tukufu ya kuzaliwa Imam Hasan al Mujtaba Alayhis Salaam na kusema kuwa tungo za kishairi zina taathira kubwa na zisizo na mfano na ni utangulizi wa kuweza malenga kubeba majukumu yao mazito. Vile vile amesisitizia udharura wa tungo za kishairi kuilinda wazi wazi na kifakhari; kambi ya haki mbele ya kambi ya batili na ubeberu wa vyombo vya kipropaganda vya kambi hiyo ya batili ulimwenguni.
Ameongeza kuwa: Tungo za kishairi za Mapinduzi ya Kiislamu ni tungo zilizojikita katika jambo hilo na zinatumikia malengo ya Mapinduzi ya Kiislamu yaani uadilifu, umoja, mshikamano, heshima ya taifa na maendeleo ya kila upande ya nchi pamoja na kujenga watu walio bora.
Ayatullah Udhma Khamenei amegusia pia uwezekano wa kutumiwa kama upanga wa ncha mbili chombo chenye taathira kubwa yaani tungo za kishairi, imma kutumika katika upande wa kumuongoa mlengwa au kwa ajili ya kumtumbukiza kwenye maangamizi na kuongeza kuwa: Leo hii kutokana na kupanuka na kuenea vyombo vipya vya kuwasiliana na watu wengi kwa wakati mmoja, baadhi ya watu wana nia ya kupotosha tungo za vijana na kuzitoa katika anga yake nzuri ya hamasa na ya kimapinduzi na kuzisukuma upande wa kutumikia utamaduni muovu ulio mbali na matukufu ya kibinadamu na ulioathiriwa na ghariza za kijinsia, kujinufaisha binafsi na kusifia mambo ya dhulma.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amewasifu baadhi ya malenga vijana kutokana na kusimama kwao kidete katika kukabiliana na anga hiyo mbaya na kusisitiza kuwa: Kusimama huko kidete kunaonesha ni namna gani vijana hao wanajali majukumu yao na leo hii utungo wowote wa kishairi ulio dhidi ya dhulma na unaotumikia malengo ya umma wa Kiislamu ikiwa ni pamoja na tungo zinazohusiana na matukio ya Yemen, Bahrain, Lebanon, Ghaza, Palestina na Syria huingia katika orodha ya tungo zenye hekima.
Vile vile amesema kuwa ni jambo lisilo na maana kumtaka malengo asijali wala asiwe na upande katika suala la kulingania haki na kupambana na batili katika tungo zake na kusisitiza kuwa: Kama malenga na msanii hatokuwa na upande katika vita vya haki na batili ajue kuwa amepoteza kivitendo kipaji na neema aliyopewa na Mwenyezi Mungu na kama atatumia kipaji chake kutumikia kambi ya batili basi ajue kuwa huo ni usaliti na jinai.
Ayatullah Udhma Khamenei amegusia pia kumbukumbu za mashambulio ya silaha za kemikali za eneo la Sardasht (yaliyofanywa na utawala wa zamani wa Iraq) na dhulma kubwa liliyofanyiwa taifa la Iran na kusema kuwa huo ni moja ya mifano muhimu na ya kusikitisha mno ambayo inabidi iakisiwe duniani kupitia lugha ya kishairi na kuongeza kuwa: Vyombo vya habari duniani na ambavyo vinadhibitiwa na Marekani, Uingereza na Wazayuni, utaviona baadhi ya wakati vinazusha makelele makubwa ulimwenguni kwa kuuliwa mnyama mmoja tu lakini katika upande wa pili vinanyamazia kimya jinai kama hiyo (ya Sardasht) na jinai nyingine mfano wake kama vile mashambulizi wanayoendelea kufanyiwa hivi sasa wananchi wa Yemen na mashambulio ya miaka ya huko nyuma dhidi ya Ghaza na Lebanon.
Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu aidha amewauliza malenga hao kwa kusema: Mtu mwenye heshima na utu anapaswa kufanya nini mbele ya kambi inayofanya jinai na uafiriti wote huo?
Ameitaja hatua ya malenga vijana nchini Iran ya kuonesha radiamali ya haraka kuhusu matukio hayo kuwa ni hatua nzuri na yenye thamani kubwa na kuongeza kuwa: Ni matumaini yangu tungo za kishairi za Mapinduzi ya Kiislamu ambazo kwa hakika zinatumikia shabaha na malengo matukufu ya Mapinduzi ya Kiislamu yaani uadilifu, utu, ubinadamu, umoja na mshikamano, uungwana na heshima ya kitaifa, maendeleo ya kila upande ya nchi na zenye kujenga watu walio bora zitazidi kunawiri siku baada ya siku.
Vile vile Ayatullah Udhma Khamenei ameelezea kuridhishwa kwake na maendeleo ya wazi wazi ya tungo za kishairi nchini Iran katika kipindi cha baada ya Mapinduzi ya Kiislamu na kusema kuwa, wigo wa tungo za kishairi nchini Iran ni mpana sana hasa kwa kuzingatia historia inayong'ara, kongwe na iliyojaa fakhari za sekta hiyo katika historia ya Iran na kuongeza kwamba: Vyombo husika kama vile vyombo vya serikali, asasi za masuala ya kiutamaduni pamoja na Shirika la Sauti na Televisheni la Jamhuri ya Kiislamu ya Iran (IRIB) vyote hivyo vinapaswa kutekeleza vizuri majukumu yao katika kadhia hiyo.
Mwanzoni mwa hotuba yake, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amewausia Waislamu kutumia vizuri baraka za mwezi mtukufu wa Ramadhani na kuzisafisha nyoyo kutokana na uchafu na kuzidi kunyenyekea mbele ya Mwenyezi Mungu Mungu na kujipinda kwa ibada na kusoma kwa wingi Qur'ani na dua za mwezi huu mtukufu.
Kabla ya hotuba ya Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu, malenga 20 wamepata fursa ya kusoma tungo zao zenye maudhui tofauti mbele ya Ayatullah Udhma Sayyid Ali Khamenei, Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu.../mh

3322279

captcha