IQNA

Tamasha la Tatu la Kiislamu la “Salam” Lafanyika Kosovo

16:56 - July 28, 2026
Habari ID: 3482546
IQNA - Tamasha la Salam 2026 limefanyika nchini Kosovo kwa ushiriki wa familia za Kiislamu, sambamba na uwasilishaji wa programu za kitamaduni na kisanii.

Pale minara ya Msikiti wa kihistoria wa Sinan Pasha inapojitokeza katika maji ya mto unaopita katikati ya mji wa Prizren, na mwangwi wa historia ya Kiuthmaniya unapochanganyika na uzuri wa kuvutia wa maumbile katika moyo wa mji wa kale, Uwanja wa Shadrvan hugeuka kuwa taswira yenye uhai inayokusanya asili ya urithi na roho ya mji huo.

Katika eneo hili, lililoko chini ya Ngome ya kihistoria ya Prizren na kandokando ya mto unaokatiza mji, misikiti, masoko ya mawe na madaraja ya kale husimama bega kwa bega, yakitengeneza mandhari iliyoifanya Prizren kuwa miongoni mwa miji mizuri zaidi ya Balkani, na mji wenye uhusiano wa ndani kabisa na utambulisho wake wa Kiislamu.

Kwa hivyo, kuchaguliwa kwa Uwanja wa Shadrvan kuwa mwenyeji wa Salam Fest 2026 hakukuwa jambo la nasibu. Kusudio la programu hii lilikuwa ni kuipa hafla hiyo upeo wa kitamaduni na ustaarabu, ambapo familia na wageni walikusanyika katika moyo wa mji huu wa kihistoria, mbele ya Msikiti wa Sinan Pasha. Hali hii iliunganisha uzuri wa mahali, utajiri wa historia na ujumbe wa Uislamu, na kuyageuza masiku hayo matatu kuwa sherehe ya maadili, familia, utamaduni na kuishi kwa maelewano.

Katika muktadha huo, Baraza la Jumuiya ya Kiislamu ya Prizren liliandaa toleo la tatu la Tamasha la Salam 2026 kuanzia tarehe 24 hadi 26 Julai katika Uwanja wa kihistoria wa Shadrvan, chini ya kaulimbiu: “Pale nyoyo zinapoungana, amani huzaliwa.”

Tukio hili la kijamii lenye upeo mpana liliwalenga wanafamilia wote, na liliunganisha shughuli za kidini, shughuli za kitamaduni, sanaa zenye maudhui, pamoja na programu za kielimu, ndani ya mazingira ya uchangamfu na uwazi.

Likisisitiza kwamba ujumbe wa taasisi za Kiislamu unafikia uwanja wa umma zaidi ya ndani ya misikiti na vyumba vya masomo, tamasha hili liliwasilishwa kupitia programu zinazokusanya pamoja makundi mbalimbali ya jamii na kuimarisha uwepo wa maadili ya Kiislamu katika maisha ya kila siku kwa kutumia nyenzo za kisasa za kielimu na kitamaduni.

Tamasha hilo lilijumuisha mfululizo wa mihadhara ya kidini na uelimishaji, sambamba na maonesho ya kisanaa na ya kimdundo, shughuli mbalimbali za watoto, pamoja na sehemu maalumu kwa madrasa za jadi za Qur’ani Tukufu iliyokuwa na matukio ya kisanaa na kielimu. Aidha, maonesho ya vyakula vya jadi yaliyoandaliwa na Idara ya Wanawake yaliwasilisha sahani za asili zilizodhihirisha vipengele vya utambulisho wa kitamaduni na kijamii wa jamii ya Kiislamu nchini Kosovo.

Tamasha hilo pia lilitoa nafasi ya mikusanyiko ya kifamilia, mawasiliano ya kijamii na kuimarisha udugu, kwa kuwakutanisha wakaazi na wageni katika mojawapo ya viwanja maarufu vya kihistoria katika eneo la Balkani ya Magharibi.

Programu ya “Tamasha la Salam 2026” ilienea kwa masiku matatu mfululizo, ikianza kwa hotuba ya Sheikh Akram Avdio, ikifuatiwa na onesho la msanii Nusrat Kurtish. Usiku wa pili ulishuhudia hotuba ya Sheikh Ardian Sajdov, sambamba na onesho la kimdundo lililowasilishwa na Salma Bektashi Meda.

Usiku wa kuhitimisha ulifungwa kwa hotuba ya Sheikh Naim Ternava, Mufti Mkuu wa Kosovo, pamoja na programu ya kimdundo.

Tamasha hili linapata umuhimu wa pekee kutokana na kufanyika kwake katika Uwanja wa Shadrvan, mkabala na Msikiti wa kihistoria wa Sinan Pasha, ambao ni miongoni mwa alama mashuhuri zaidi za Kiislamu nchini Kosovo. Eneo hilo liko katikati ya mji wa kale wa Prizren, chini ya ngome ya kihistoria na kandokando ya mto unaougawa mji katika sehemu mbili. Hali hii hulipa tukio hilo tabia ya kipekee ya kitamaduni inayounganisha uasilia wa mahali, uzuri wa maumbile, na ujumbe wa kitamaduni na kidini wa tamasha hilo.

Prizren ndiyo mji mkuu wa kihistoria na kitamaduni wa Waalbania katika Balkani ya Magharibi, na ni miongoni mwa miji maarufu zaidi ya Kiislamu katika eneo hilo. Mji huo una makumi ya misikiti ya kale na ya kisasa, masoko ya Kiuthmaniya, madaraja ya mawe na minara ambayo yamekuwa sehemu isiyotenganishwa na utambulisho wake wa kimuonekano, hali iliyoupatia jina la utani la “Istanbul Ndogo.”

Tamasha la Salam 2026 linaakisi maono ya Baraza la Jumuiya ya Kiislamu ya Prizren ya kugeuza matukio ya kijamii kuwa jukwaa la kupandikiza maadili ya Kiislamu, kuimarisha nafasi ya familia, na kuwaunganisha watoto na vijana na utambulisho wao wa kidini na kitamaduni kupitia programu zinazochanganya elimu, burudani yenye maudhui, sanaa za hali ya juu, na ushiriki wa kijamii.

Vilevile, tamasha hili linatoa mfano wa maendeleo katika matumizi ya maeneo ya kihistoria kwa madhumuni ya kitamaduni na da‘wah, jambo linaloongeza uwepo wa taasisi za Kiislamu ndani ya jamii na kuthibitisha uwezo wake wa kuzungumza na makundi mbalimbali kwa mbinu za kisasa zinazochanganya urithi na ubunifu.

3498435

Kishikizo: kosovo waislamu
captcha