IQNA

Ansarullah yakanusha madai ya Saudia kuhusu kushambuliwa Makkah

7:37 - October 30, 2016
Habari ID: 3470642
Harakati ya Ansarullah nchini Yemen imekanusha madai ya Saudia kuwa imeshambulia msikiti wa Makkah.
Msemaji wa Harakati ya Kiislamu ya Ansarullah nchini Yemen amesema kuwa, madai yanayotolewa na utawala wa Aal-Saud kwamba harakati hiyo na jeshi la Yemen imeshambulia msikiti wa Makkah, ni njama za kuamsha hisia za Waislamu duniani kwa lengo la kuomba msaada toka kwao baada ya kushindwa vita.
Mohammad Abdus Salam, amewataka Waislamu duniani kupuuza madai hayo ya uongo yanayoenezwa na muungano vamizi wa Saudia sanjari na kuyataja kuwa yasiyo na maana. Abdus Salam amesema kuwa, Wayemen hawahitaji hisia za kidini wala za Kiarabu na kwamba jeshi la taifa hilo licha ya mashambulizi ya kila upande yanayotekelezwa na Saudia na waitifaki wake ikiwemo Marekani na utawala haramu wa Israel na kadhalika hasara kubwa iliyolenga miundombinu, hawajawahi kushambulia hata taasisi moja ya Saudia, achilia mbali maeneo matakatifu ya kidini kama vile Nyumba ya Mwenyezi Mungu al-Kaabah.
Itafaa kuashiria kuwa, Alkhamis iliyopita, jeshi la Yemen liliushambulia kwa kombora aina ya Burkan 1 uwanja wa ndege wa kimataifa wa Mfalme Abdulaziz mjini Jeddah, magharibi mwa Saudia na kusababisha hasara kubwa. Duru za ndani nchini Saudia zinaarifu kwamba, kufuatia shambulio hilo, utawala wa Aal-Saud ulipatwa na wasi wasi mkubwa na hivyo asubuhi ya Ijumaa ukadai kuwa, kombora moja lilirushwa na jeshi la Yemen kutoka mji wa kaskazini mwa Saada kuelekea mji mtukufu wa Makkah, huku jeshi la Yemen likishangazwa na madai hayo yenye lengo la kuibua hisia za Waislamu duniani.
Kufuatia madai hayo, baadhi ya duru nchini Saudia zilifichua kuwepo njama za watawala wa Aal-Saud za kutekeleza shambulizi dhidi ya maeneo matakatifu ya kidini na kisha kuitwisha lawama harakati hiyo ya Kiislamu ya Answarullah nchini Yemen, ambayo hadi sasa imeweza kufelisha malengo machafu ya Saudia na waitifaki wake ndani ya Yemen.
3541305
captcha