Mwambata wa Utamaduni wa Iran mjini Dar es Salaam ameliambia Shirika la Habari la IQNA kuwa, matembezi hayo yalifanyika Jumanne katika eneo la Stone Town mjini Zanzibar. Baada ya hapo washiriki walielekea katika Msikiti wa Hujjatul Islam na kusimamisha sala ya Jamaa.
Kabla ya Sala kulikuwa na mashairi ya maombolezo na baada ya hapo hadhirina wakasikiliza hotuba ya Maulana Sheikh Hemedi Jalala Kiongozi Mkuu wa Hawzatul Imam Sadiq AS ya Kigogo, Dar es Salaam.
Katika hotuba yake, Sheikh Jalala aliashiria fadhila na sifa kipekee za Bwana Mtume Muhammad SAW huku akitoa wito kwa Waislamu kuungana chini ya bendera ya mapenzi kwa Mtume SAW na Ahlul Bayt AS wake watoharifu. Sheikh Jalala amesisitiza kuwa, kuibua migongano ya kimadhehebu ni njama ya maadui wa Uislamu. Kikao hicho kilimalizika kwa sala iliyowashirikisha Waislamu wa madhehebu ya Sunni na Shia.