IQNA

Rais wa Iran azungumza na mwenzake wa Afrika Kusini kuhusu kadhia ya Shahidi Soleimani

20:05 - January 10, 2020
Habari ID: 3472359
TEHRAN (IQNA) - Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa anataraji kwamba Wamarekani watahitimisha hatua zao ghalati, lakini iwapo watatekeleza hatua nyingine iliyo dhidi ya maslahi ya Iran, basi watapata jibu kali mkabala.

Rais Rouhani ameyasema hayo katika mazungumzo yake ya simu na Rais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini ambapo sambamba na kubainisha kwamba chanzo cha masuala mengi hatari katika eneo kinatokana na vikwazo haramu, ameongeza kwamba anataraji kuwa nchi zote marafiki wa Iran zitachukua msimamo chanya kuhusiana na hatua hizo zilizo kinyume cha sheria za Washington na hatimaye waweze kuirejesha nchi hiyo kwenye mkondo wa sheria. Rais wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran amesema kuwa kuchukuliwa na nchi zote msimamo wa kulaani mauaji ya kigaidi dhidi ya Luteni Jenerali Qassem Soleimani ni suala muhimu sana, amesisitiza kuwa ni lazima Wamarekani wafahamishwe kwamba ulimwengu haukubaliani nao kuhusiana na hatua zao za kijinai. Akibainisha kuwa katika miaka ya hivi karibuni Luteni Soleimani aliendesha mapambano kwa muda mrefu dhidi ya makundi tofauti ya kigaidi hususan genge la kigaidi la Daesh (ISIS) amesema kuwa jinai ya kumuua kigaidi shakhsia huyo muhimu imewaunganisha wananchi wote wa Iran mbele ya nchi vamizi.

Kadhalika Rais Hassan Rouhani wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran ameitaja Afrika Kusini kama nchi rafiki ambayo siku zote imekuwa kando na Tehran na kuongeza kuwa, nao wananchi wa Iran siku zote wamekuwa na mtazamo wa kirafiki kwa wenzao wa nchi hiyo ya Afrika hususan katika kipindi cha ubaguzi wa rangi. Kwa upande wake Rais Cyril Ramaphosa wa Afrika Kusini sambamba na kutoa mkono wa pole kwa serikali na wananchi wa Iran kufuatia kuuawa shahidi Luteni Jenerali Qassem Soleimani, na kuyataja mauaji hayo kuwa ya udhaifu, amesema kuwa habari ya kuuawa Soleimani ambaye alikuwa kipenzi cha watu, iliibua mshtuko na amelaani vikali mauaji hayo ya kigaidi ya Marekani.

113261

captcha