Katika barua hiyo aliyomwandikia Antonio Guterres Ijumaa, Zarif ameashiria nukta muhimu kadhaa kuhusiana na kujitoa kinyume cha sheria Marekani katika makubaliano ya nyuklia ya JCPOA, vikwazo vya upande mmoja ilivyoiwekea Iran na ukiukaji mkubwa na wa mara kwa mara inaofanya wa Hati ya Umoja wa Mataifa na hasa kifungu cha 25, hatua ambazo ni tishio kwa itibari ya umoja huo pamoja na amani na usalama wa kimataifa.
Barua hiyo ni ya pili kuandikwa na Zarif kwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika kipindi cha miezi miwili sasa.
Tarehe 12 Machi mwaka huu pia, Waziri wa Mambo ya Nje wa Jamhuri ya Kiislamu ya Iran alimwandikia barua Antonio Guterres ambayo nakala yake ilitumwa kwa wakuu wa jumuiya za kimataifa na mawaziri wa mambo ya nje wa nchi zote duniani, akisisitiza na kutilia mkazo ulazima wa kuondolewa vikwazo vya upande mmoja vya Marekani dhidi ya Iran ili kuiwezesha Tehran kukabiliana na janga la COVID-19.
Dakta Zarif amemwandikia barua Katibu Mkuu wa UN hapo jana Mei 8, ukiwa umetimia mwaka wa pili tangu Marekani ilipojitoa kinyume cha sheria katika makubaliano ya nyuklia ya JCPOA.
Tarehe 8 Mei, 2018 Rais Donald Trump wa Marekani alikiuka ahadi na majukumu ya nchi yake katika makubaliano ya nyuklia ya JCPOA alipochukua hatua ya upande mmoja ya kujitoa kwenye makubaliano hayo ya kimataifa na kurejesha tena vikwazo vya nyuklia dhidi ya Iran.
Hatua hiyo ya Trump imepingwa na kulaaniwa vikali ndani ya Marekani na katika uga wa kimataifa.